Tuesday, 19 January 2016

Jezuu 8 AL HAJJI---Kujenga uongofu katika nyoyo za vijana-----








 Latest : For English Translation Please Press HERE








“Kwa yakini nyumba ya kwanza iliyowekwa na kwa ajili ya watu (kufanya ibada) ni ile iliyoko Makka, yenye baraka na uwongozi kwa ajili ya walimwengu wote, Humo mna Ishara zilizowazi (za kuonesha utukufu wake na ukongwe wake miongoni mwa hizo ni) mahali alipokuwa akisimama Ibrahim; na kuwa anayeingia (Nchi hiyo) anakuwa katika Salama; na kuwa Allah amewawajibishia watu wafanye Hija kwenye Nyumba hiyo; wale wawezao kufunga safari ya kwenda huko”.











“(Tukawaambia): Na utangaze kwa watu habari za Hija, watakufikia, (wengine) kwa miguu na (wengine) juu ya kila mnyama aliyekonda (kwa machofu ya njiani) wakija kutoka katika kila njia ya mbali, ili washuhudiye manufaa yao na ili wakithirishe kulitaja jina la Allah katika siku zinazojulikana na fadhila zake juu ya yale aliyowaruzuku, nao ni wanyama wenye miguu minne, na kuleni katika wanyama hao na mlisheni mwenye shida aliyefakiri.”
Hija ni nguzo ya tano katika nguzo za Kiislamu na ndiyo iliyo na vitendo vigumu zaidi kuliko nguzo zote nyingine. Basi unapotaka kwenda kuhiji na kufanya Umra au kufanya Umra tu ili upate hadhi ya kujikaribisha na Allah na ujipeleke kwenye upepeo wa Rehema zake na uzunguke Al-Kaaba yenye kuheshimika na ufanye saayi baina ya Safa na Al-marwaa na kupata hadhi ya kuzibusu zile sehemu tukufu ambazo amezipitia Mtume Salallahu Alayhi Wasalam (ametembea juu yake) pamoja na watu wa mwanzo aliosuhubiana nao yaani Masahaba na waliofuata njia zao, Mataabiin. Na kwa hao ilibadilika hali kutoka giza kwenda kwenye elimu na kutoka katika Ushirikina kwenda kwenye Tawhiid (kumpwekesha Allah Subhanahu Wataala ).
Ukitaka kwenda kuhiji au Umra kwa uwezo wa Allah na Tawfiiq yake basi na ufanye kama ifuatavyo:
Isahihishe niya yako hata iwe kutoka kwako huko ni kwa kutaka radhi yake Subhanahu Wataala. Wala usimshirikishe pamoja naye mwingine (kujionesha kwa watu kuwa sasa wewe pia umekuwa Al-Hajji au kwenda huko kwa kufanya biashara na mengineyo). Unuiye kufanya Umra na kuhiji au kufanya Umra tu au Kuhiji tu. Kwa hali yoyote inakulazimu utiye niya kabla hujaondoka na vile vile inakulazimika urudishe haki zote za watu zilizo juu yako. Iwapo huwezi kuzirudisha kwa wakati huo basi andika karatasi rasmi ya kishariya kuwa ukipatwa na mauti katika Hija yako hiyo walipwe hao wenye haki zao. Hakikisha wasiya wako huo utatekelezwa (kwa kuacha kitu kinachofidiya hizo haki na kumwakilisha mtu madhubuti) kwani mja yuko katika kabdha ya Muumbaji wake Subhanahu Wataala (wakati wowote akimtaka atamchukua).
Hakuna budi safari yako ima iwe kwa gari au kwa ndege na kwa hali zote mbili Umra inayoanziwa Dhul huleifa (sasa inaitwa Abyaar Ali) ni bora zaidi, kuliko kuanzia kwengine kwani inayoanziwa Dhul huleifa inakuwa mfano wa Mtume Salallahu Alayhi Wasalam kisha ni Mikaati iliyo mbali zaidi kuliko zote na kila Ihraam ikiwa ndefu inazidi thawabu.
Iwapo utakwenda kwa gari basi nenda moja kwa moja mpaka Madina Al-Munawarah, ama ukiwa umesafiri kwa ndege na umeteremka Jedah basi nenda zako moja kwa moja Madina bila ya kuingia Makka.
Ukifika Madina kwa uwezo wake Subhanahu Wataala ukithirishe kumsalia na kumsalimia Mtume Salallahu Alayhi Wasalam na uingie msikiti wa Mtume Salallahu Alayhi Wasalam unaohishimika baada ya kuweka mizigo yako hapo mahala ulipofikilia.
Ukiingia msikitini usali rakaa mbili “Tahiyyatul Masjid” na ukiweza kusali hizo rakaa mbili pamoja na Salaa zote katika asli ya msikiti alioujenga Mtume Salallahu Alayhi Wasalam fanya bidii usali hapo kwani nafsi inahisi raha zaidi, lakini hakuna kitu ukisali popote katika Msikiti huo kwa sababu Mtume Salallahu Alayhi Wasalam amesema: Kila kilicho wasiliana na msikiti wake hukumu yake sawa sawa na msikiti wake hata ukafika San’aa. Baada ya kusali hizo rakaa mbili uwende kwa adabu na unyenyekevu pale lilipo kaburi la Mtume Salallahu Alayhi Wasalam usimame mbele yake kisha useme:
 (السلام عليك يارسول الله السلام عليك يا نبي الله ورحمة الله وبركاته أشهد أنك رسول الله حقاً وأنك بلغت الرسالة وأديت الأمانة ونصحت الأمة وجاهدت في الله حق جهاده فجزاك الله عن الإسلام والمسلمين خيراً وآتاك الوسيلة والفضيلة والدرجة العالية الرفيعة وأرجو يا رسول الله أن أكون من أهل شفاعتك يوم القيامة )
Baada ya hapo utasogea upande wa kulia kidogo, na utamtolea Salamu Assadiq (Abu Bakr RA) na utasema :
( السلام عليك يا صاحب رسول الله في الغار ويا خليفته على المسلمين السلام عليك ورحمة الله وبركاته أشهد أنك خلفت رسول الله وقمت بواجبك ونصحت للأمة فجزاك الله خيراًَ )
Kisha utasogea kuliani kwako kidogo na utamsalimia Al-Faaruuq (Omar bin Al-Khattaab RA) na useme:
( السلام عليك يا أبا حفص السلام عليك يا أمير المؤمنين أشهد أنك أمرت بالمعروف  ونهيت عن المنكر واجتهدت لأمة محمد نصحاً وإخلاصا فجزاك الله خيرا )
Baada ya hapo uondoke na tahadhari usiguse kwa mkono wako kitu au uchezee kitu usije ukajiharibia nafsi yako na madhehebu yako.
Kwani madhehebu ya Ibadhi imesafika wala haikuchafuliwa na chochote nayo ni kilele katika adabu na wala haichukuwi mafundisho isipokuwa kwa Allah Subhanahu Wataala na Mtume wake Salallahu Alayhi Wasalam.
Na ukae huko Madina kama utakavyojaaliwa (utakavyoweza) na wala hakushurutishwi kukaa muda fulani na ukiwa huko uzidishe kusali katika msikiti wa Mtume Salallahu Alayhi Wasalam kwani sala moja hapa ni sawa na sala elfu kwa hiyo usipoteze fursa hiyo. Vile vile utembelee msikiti wa Quba na usali ndani yake kwani Allah Subhanahu Wataala ameteremsha juu yake kauli yake katika Qurani tukufu:
التوبة: ١٠٨
“Msikiti uliojengwa juu ya msingi wa kumcha Mungu tangu siku ya kwanza (ya kufika Mtume Madina) unastahiki zaidi wewe usimame humo. Humo wamo watu wanaopenda kujitakasa. Na Allah anawapenda wajitakasao.”
Wasema wanavyuoni kuwa Mtume Salallahu Alayhi Wasalam aliwauliza watu wa msikiti wa “Quba”: Kwa nini Allah kawasifu? Wakamjibu: tulikuwa tukifuatishia maji (baada ya kujipangusa kwa ) mawe iwapo tukienda choo kidogo au kikubwa.
Na inapendelewa kuzuru makaburi ya Mashahidi wa Vita vya “Uhud” na uwasalimie na uwaombee maghufira. Inataka wakati huo ukumbuke mapambano yaliyotokeya hapo baina ya Mtume Salallahu Alayhi Wasalam na Washirikina wa Quraish na wengineo Allah Subhanahu Wataala akawashinda ushindi mbaya. Baada ya kuwafanyiya Waislamu mtihani mara ya kwanza na wakashindwa (na maadui zao kwa sababu hawakufaulu huo mtihani waliopewa kwa kutofuata amri ya Mtume Salallahu Alayhi Wasalam) kisha ukarudi ushindi kuwa wao (Waislamu).
Basi ujue kuwa Dini hii haikutufikia kwa urahisi bali imetufikia kwa juhudi kubwa na jihadi ya tabu na uchungu mkubwa na leo Waislamu waichezea na wabomoa kile kilichohifadhiwa na wale wenye ikhlasi (basi huu ni msiba mkubwa sana)  إنا لله وإنا اليه راجعون
“Sisi ni wa Allah na kwa hakika kwake tunarejea”.
Unapoazimia kwenda Makka Al-Mukarrama ni lazima utakuwa katika hali moja ya hali tatu zifuatazo:
Iwe umekusudia kufanya Umra kisha uvue Ihram upumzike halafu uvae Ihram ya Hija.
Iwe umekusudia kufanya Hija peke yake.
Iwe umekusudia kuchanganya baina ya Haji na Umra kwa Ihram moja.
Hali hizi tatu hazitokei isipokuwa katika miezi ya Hija nayo kuanzia siku ya mwanzo wa Shawal (Mfungo Mosi) mpaka siku ya nane ya mwezi wa Dhil Hija (Mfungo tatu) na katika hali zote tatu ufanye kama ifuatavyo: Uoge kama unavyooga janaba kisha utawadhe tena uvae nguo mbili, ambazo hazikushonwa moja uifanye kikoi na ya pili uivae juu ujizungushie mwilini na wala usiziunganishe kwa kuzipiga fundo au kwa shindano na ziepushe kuguswa na manukato halafu usali rakaa mbili ya “Ihraam” usome katika rakaa ya mwanzo (baada ya sura Al-Fatihah):
( قل يا أيها الكافرون )
Na katika rakaa ya pili baada ya Al-Hamdu:
( قل هو الله احد )
Kisha unaweka niya baada kutoa Salamu useme:
 ( لبيك اللهم لبيك لبيك لا شريك لك لبيك إن الحمد والنعمة لك والملك لا شريك لك)
Na ukiwa mutamattii (yaani ukiwa katika hali ya kwanza katika zile hali tatu) uzidishe kwa kusema:
( بعمرة تمامها وبلاغها عليك يا الله )
Na ukiwa mufrid (yaani katika hali ya pili) uzidishe kwa kusema:
 ( بحجة تمامها وبلاغها عليك يا الله )
Na ukiwa umechanganya baina ya Hija na Umra (hali ya tatu): uzidishe kwa kusema:
 ( بحجة وعمرة تمامهما وبلاغهما عليك يا الله )
Useme haya mara tatu halafu uongeze kusema:
 ( اللهم إني أسألك رضاك والجنة وأعوذ بك من سخطك والنار لا إله إلا أنت وصلى الله على رسوله سيدنا محمد وآله )
Ufanye haya yote ukifika “Dhul-Huleifa.” Na ukifanya haya Madina hapana kitu (inafaa).
Ama kuoga ni rahisi kwako na ni utaratibu kwako kuoga katika nyumba uliofikia huko Madina na uvae nguo ya Ihram huko huko. Ama kutia niya ya Ihram na kufanya Ihram ni bora kufanya haya Dhul-Hulaifa ikiwa wewe ni katika mahujjaji wanaosafiri bara, ama ukiwa katika mahujjaji wanaosafiri angani usiharakishe kutia Ihram mpaka uhakikishe kuwa umepata okey katika ticket yako kwa sababu ukifanya Ihram nawe hukusafiri utabakia katika tabu na mashaka (kwani Ihraam ina masharti yake usipoyashika itakubidi damu yaani uchinje).
Wala haifai kuihalalisha hiyo Ihraam mpaka umalize vitendo vya Hija au Umra na iwapo utahakikisha usafiri wako (kwa kupata okey katika booking yako) basi sali rakaa mbili katika kiwanja cha ndege utakachosafiria na utie Ihram baada ya hizo rakaa (useme: Labbaika Allahuma Labbaika n.k). Na utawakali kwa Allah, na utahadhari ewe mwenye Ihram usije ukakata unywele au kucha au kufanya kazi yoyote ambayo inaweza ikakusababishia kuumia ukatoka damu au usije ukagusa mafuta mazuri au usijikumbushe jimai kwani mambo haya yote huharibu Ihramu yako na kusabibishia damu yaani kuchinja mbuzi au kondoo katika ardhi ya Al-haram. Na wala usighafilike kufanya “Talbiya”   (“Labbeika”…)  baina ya wakati na mwingine bila ya kukazania sana (yaani kufanya talbiya moja kwa moja) na hakika talbiya ni katika vitendo muhimu sana vya Hija basi usiikate mpaka utakapoiona Baitul Al-Haram.
Ufikapo Makka Al-Mukarrama teremka kwanza katika mahala ambapo utafikia ili ushushe mizigo yako (Ipo nyumba hapo Makka, Bait Ribaat, imeekwa wakfu na baadhi ya watu wema kwa mafakiri wa Kiibadhi kwa hiyo haifai kwa asiye Muibadhi kukaa ndani yake na vile vile haifai kwa Muibadhi aliye tajiri kukaa humo kwa sababu kukaa kwao humo kutaibadilisha  wasiya iliyoekwa na mwenye kuiweka wakfu. Kwa sababu aliemkusudia Allah katika kitendo chake basi asimwendee kinyume kwa cho chote.)
Ukisha weka mizigo yako jitie udhu na uwende Masjid Al-Haram, na utakapoiona Al-Kaaba ukate talbiya yako na useme:
 ( اللهم إن هذا بيتك وأنا عبدك فأنلني فيه مناي واغفر ذنبي ووفقني للعمل بطاعتك وصلى الله على سيدنا محمد وآله )
Kisha uende kwenye Hajar Al-aswad ukilifikia libusu ikiwezekana bila ya kuudhi au kuudhiwa ama sivyo inakutosha kulishika kwa mkono wako na hata iwapo hukuweza hivyo basi lifanyie ishara kwa mkono wako kwani Mtume Salallahu Alayhi Wasalam aliliashiria kwa bakora iliyokuwa mkononi mwake. Kisha uanze kuzunguka Al-Kaaba (Tawaaf) kabla hujauona mlango (wa kaaba) uzunguke mara saba, na mzunguko mmoja (“shawt”) ni kutoka Hajar Al-aswad mpaka Hajar Al-aswad. Lazima udhibiti mizinguko yako  kwani ikiwa hukuihifadhi inakubidi uirudie tena upya. Na haitimii tawaaf mpaka uwe na hakika nayo na usome katika mizunguko yako yote:
( سبحان الله والحمد لله ولا إله إلا الله والله أكبر ولا حول ولا قوة إلا بالله )
Masahaba radhi za Allah ziwe juu yao walikuwa hawazidi juu ya maneno hayo. Iwapo utaomba kwa Dua unayoijua hapana kitu(inafaa) lakini kinachokatazwa ni kushika kitabu cha Dua chenye Dua ya mzunguko wa kwanza (shawt)  na Dua ya shawt ya pili mpaka shawt ya saba basi hivo ndivyo wafanyavyo wengi katika mahujjaji wala hawajui kitu gani wanasoma na wana Imani kuwa tawaaf haitimii isipokuwa kwa kusoma Dua hizo. Na msingi wa kisheria unasema ukiomba Dua uliokuwa huijui maana yake basi hutakabaliwi (hupokelewi). Twamuomba Allah amchunge kwa Rehema zake yule anaemkusudia yeye tu na akafanya Ikhlaas kwa ajili yake.
Na kwa hakika inapendelewa useme upitapo baina ya “Rukni Al-yamaniy” na Hajar Al-aswad useme:
Vile vile inapendelewa upitapo kwenye Al-Miizaab useme:
 ( اللهم إني أسألك الراحة عند الموت والعفو عند الحساب والفوز بالجنة والنجاة من النار )
Na upitapo Rukn Al-yamaaniy uiguse kwa mkono wako bila ya kuibusu kwani linalobusiwa ni Hajar Al-aswad tu kwa mujibu wa Sunna. Na umalizapo kuzunguka (Al-Kaaba) mara saba umshukuru Allah Subhanahu Wataala kwa kukupa tawfiiq (ya kufanya vitendo hivyo vitukufu). Ikiwa utaweza kusimama kwenye huo mlango (wa Al-Kaaba) na uligusanishe tumbo lako ukutani na ukamate kwa mkono wako chini ya mlango na umuombe Allah kadiri utakavyojaaliwa kwani inahimizwa kufanya hivyo. Na Dua iliyo bora zaidi ni kumuomba Allah akusamehe katika Dunia na Akhera kwani Dua hiyo inakusanya yote. Aliyemsamehe Allah Subhanahu Wataala katika Dunia yake na Akhera yake ataka nini zaidi ya hayo?
Kisha sali rakaa mbili nyuma ya Maqamu Ibrahim na hizo ni rakaa mbili za tawaaf (kuzunguka Al-Kaaba) faridha na ukiwa huwezi kusali nyuma ya Maqamu Ibrahim kwa sababu ya msongamano wa watu basi unaweza ukasali mahali po pote katika msikiti huo. Usome katika rakaa mbili baada ya sura Al-faatihah: Qul Yaa Ayuha lkaafiruun (rakaa ya kwanza) na Qul Huwa Allahu Ahad (rakaa ya pili). Na umuombe Allah kiasi utakavyojaaliwa. Kisha unywe maji ya Zam Zam mpaka ushibe maji na ujirushie kichwani kwani ni baraka na kuifuata Sunna ya Mtume Salallahu Alayhi Wasalam.
Kisha baada ya hayo yote uende kufanya Saayi (mwendo baina ya Safa na Marwa) uanze na Safa na usome ukipanda juu ya kilima chake:
 ( أبدأ بما بدأ الله به )
البقرة: ١٥٨
“Hakika Safa na Marwa (Majabali mawili yanayofanyiwa ibada ya kusai huko Makka) ni katika alama za kuadhimisha Dini ya Allah. Basi anayehiji kwenye nyumba hiyo au kufanya Umra, si kosa kwake kuvizunguka (vilima) hivyo viwili; na anayefanya wema (atalipwa) kwani Allah ni Mwenye shukurani na Mjuzi (wa kila jambo)”.
Wanavyuoni wamefanya utafiti katika Aya hii wakasema: kwa sababu gani Allah amesema: “Si kosa kwake kuvizunguka (vilima hivyo viwili) pamoja ya kuwa tawaaf ni sunna, wakaona kuwa katika wakati wa ujahiliya yalikuweko masanamu mawili katika vilima viwili hivyo yaitwa “Asaaf” na “Naailah”. Ulipokuja Uislamu wakaona taabu Waislamu kufanya Saayi baina ya hiyo milima miwili wasije wakafata mfano wa  washirikina. Ndipo ilipoteremka Aya hii kuwaambia kuwa Ushirikina umeondoka na umetoweka na sasa huu Uislamu katika nguvu yake na ukubwa wake.
Na upandapo kilima cha Safa useme:
 ( لا إله إلا الله وحده لا شريك له، له الملك وله الحمد وهو على كل شيء قدير، تائبون آيبون عابدون لربنا حامدون، لا إله إلا الله وحده صدق وعده ونصر عبده وهزم الأحزاب وحده )
Baada ya kusema hayo uteremke kuelekea Marwa na ukifika katikati ya bonde na leo hakuna athari ya bonde isipokuwa imewekwa ishara ya taa za kijani sakafuni inayoonyesha mwanzo wa wadi na mwisho wa wadi (bonde).
Ukifika mahali hapa kimbia kidogo kidogo (polepole) kama uwezavyo siyo kupiga mbio sana na useme:
 ( اللهم اجعل ممشاي هذا كفارة لكل مشي كرهته مني اللهم إني أسألك العمل بما ترضى والفوز بالأخرى ، اللهم اغفر وارحم  وتجاوز عما تعلم )
Na useme katika Saayi yote kama ulivyosema katika tawaaf na unamalizika mzunguko (shawt) wa kwanza katika Marwa na inaanza hapo shawt ya pili na vivyo hivyo mpaka zikamilike shawt saba, unaanza katika Safa na unamalizia katika Marwa, na uelekee Al-Kaaba ukifika Safa na Marwa.
Mwanamke asipande juu ya kilima cha Safa wala kilima cha Marwa wala asikimbie baina ya alama mbili (za kijani) kwani haya yote makhsusi kwa wanaume. Ama mwanamke anatakiwa asimame chini ya As-Safa na Al-Marwa na atembee mwendo wa kawaida baina ya alama mbili (za taa ya kijani) kama anavyotembea katika Saayi iliyobakia, na haya yote ni kwa ajili ya kuhifadhi sitara yake kwani anawajibikiwa kuihifadhi katika hali zake zote wala hakuruhusiwa kuonesha kitu cho chote katika mapambo yake (sehemu zake za mwili zinazovutia) katika hali yoyote isipokuwa kuruhusiwa kwake kuacha wazi uso na mikono miwili katika hali ya Ihram na kuzifunika sehemu hizo katika nyakati nyinginezo ni bora.
Ukishamaliza kufanya Saayi (mwendo baina ya Safa na Marwa) ukate nywele lakini ukizinyoa ni bora zaidi. Na huko kukata nywele ni kupunguza baadhi ya nywele katika kichwa chako. Ama mwanamke yeye apunguze kadiri ya kidole kimoja au vidole viwili katika ncha ya nywele zake wala asipunguze zaidi ya hivyo. Mwanamme haruhusiwi kukata au kupunguza kitu katika ndevu zake kwani kupunguza ndevu ni haramu, kwani haiwi katika utiifu wa Allah kufanya maasi (huko kukata ndevu). Na bora muhrim akatwe nywele na asiyekuwa muhrim wako vinyozi hapo nje ya Al-Haram; kisha ukishanyolewa wewe mwanamme uchukue mkasi umkate mkewo au ndugu yako na mwanamke amkate mwanamke mwenzake wala asimkate nywele zake mwanamme isipokuwa akiwa mahrim yake kama baba, ndugu, ami mjomba wake n.k. Na mpaka hapa imemalizika Umra kwa tawfiki ya Allah na anaejitahidi hupata tawfiki.
Mwenye kuihalilisha Ihram yake (Mutamatii) na akawa amepumzika kuingojea Hija huvua ngua zake za Ihram na hufanya kila alichoharimishiwa katika hali ya Ihram. Ama mwenye kuchanganya Umra na Hija (Al-Muqrin) hubakia katika Ihram yake (nguo zake za Ihram) kwani yeye bado ni Muhrim na anaharamishiwa kila alichoharimishiwa Muhrim. Mpaka itakapofika siku ya nane ya Dhil Hija. Yule aliyejihalilisha na Ihram yake (Mutamatii) ya Umra sasa anafanya Ihraam ya Hija huko Al-Bat-haa au katika Masjid Al-Haraam au katika nyumba aliyofikia. Kisha wanaelekea Mahujjaji wote huko Muna baada ya kupindukia jua na hawatasali Sala ya Adhuhuri na Sala ya Al-asiri mpaka wafike Muna wazichanganye (jama’an) na wazisali rakaa mbili mbili (qasraan).
           
Mwenye kutia niya ya kuhiji tu (Al-Mufrid) hubakia katika Ihraam yake. Iwapo atafika Makka kabla ya tarehe 8 nane Dhil Hija hatofanya tawaaf (kuzunguka Al-Kaaba) bali atabakia na Ihraam yake na atasali katika Masjid Al-Haram.
Usiku wa kuamkia tarehe 9 tisa Dhul Hajji ulale hapo Muna na usali Sala tano hapo (kama tulivyosema kabla kuwa uchanganye Adhuhuri na Al-Asiri  na kadhalika Al-Maghrib na Al-Ishaa  katika tarehe 8 Dhil Hajji na Sala ya Al-Fajiri mnamo tarehe 9 Dhil Hija). Ufikapo Muna useme:
 ( اللهم إن هذه منى وهي مما دللت عليه من المناسك وأسألك أن تمن علي فيها وفي غيرها بما مننت به على أوليائك وأصفيائك فها أنا ذا عبدك بين يديك وفي قبضتك وصلى الله على سيدنا محمد )
Na asubuhi ya siku ya tisa nayo ndiyo siku ya Arafa baada ya kwisha toka jua (sio kabla ya kutoka jua) uende huko Arafaat na usimame hapo (Wuquuf) na useme:
{اللهم إليك قصدت وإليك صمدت وما عندك أردت أسألك أن تبارك لي في رزقي وأن تلقيني في عرفات حاجتي وصلى الله على سيدنا محمد وعلى آله وصحبه وسلم{
Usiwache kusoma talbiya baina ya wakati na mwingine na baada ya kusali Sala za faridha (usome talbiya) na ukiona mjumuiko wa watu (vile vile usome talbiyah) kila ukizidisha talbiyah ni kheri kwako na katika hadithi:  (الحج العج والثج)   maana yake Hija ni kupandisha sauti kwa kufanya talbiyah (العج) na kumwaga damu ya mnyama unaemtoa sadaka (الثج) .
Ukifika Arafaat napo ni mahala panapojulikana kuna sehemu hapo inaitwa “Arina” iko jirani na Arafaat anaesimama hapo huyo hana Hija (Hija yake imekuwa baatil) basi na watahadhari wasiojua wasije wakafanya kosa hilo, wengi katika wanaowachukua Mahujjaj (Muqawiliin) huwapeleka huko hawajali kufanya kosa hili kwa hoja ya kukimbia fujo ya watu (iliyoko Arafaat). Hii ni khiyana na kitu kinachompasa anaekwenda kuhiji aulize na asiwe mjinga ili ajiepushe na mambo yanayoharibu Hija yake.
Kusimama Arafaat (Wuquuf bi Arafaat) ni nguzo ya pili ya Hija baada ya Al-Ihraam na ukifika hapo useme:
 (اللهم هذه عرفات فاجمع لي فيها جوامع الخير كله واصرف عني فيها جوامع الشر كله وعرفني فيها ما عرفت أولياءك وأصفياءك وصلى الله على سيدنا محمد )
Kisha ujitayarishe kwa msimamo (Wuquuf bi Arafaat) kwanza ule na kisha utawadhe na likishapindukia jua huo ndio wakati wa Wuquuf umewadia na usali Adhuhuri na Al-Asiri pamoja na kuzifupisha (jama’an qasraan) Sala ya Jamaa. Halafu usimame kumuomba Allah Subhanahu Wataala akughufirie madhambi yako na akufutie makosa yako na akutekelezee haja yako kwani Allah Subhanahu Wataala yu Karimu hamrudishi katika siku hii mwenye kumuomba kwa Ikhlasi ikiwa hakumuomba Allah haja isiyofaa kuombwa. Na kila msimamo huo ukiwa wima ni bora zaidi na ikiwa huwezi ukae na ikiwa huwezi ujinyooshe.
Msimamo huko Arafaat maana yake: Kuomba haja zako kutoka kupindukia kwa jua mpaka kuzama jua. Unatumia wakati huu wote katika kumtaja (kumkumbuka) Allah, kumuomba, na kunyenyekea kwake akukubalie maombi yako, uhudhurishe madhambi yako uliyoyafanya (uyakumbuke na umwombe Subhanahu Wataala akughufurie) na ujihisabu nafsi yako na unyenyekee kwake Subhanahu Wataala akutakabalie na uzidishe kumdhukuru Allah Subhanahu Wataala kwa kusema:
( لا إله إلا الله وحده لا شريك له )
Kwani hiyo ni katika Dua iliyo bora kuliko zote kama ilivyokuja katika hadithi:
 ( أفضل ما قلته وقال النبيون قبلي لا إله إلا الله وحده لا شريك له )
Bora ya niliyoyasema mimi na waliyoyasema Manabii kabla yangu ni:
 ( لا إله إلا الله وحده لا شريك له )
Na wala usijishughulishe na lolote katika mambo ya Dunia isipokuwa lenye dharura kwani hiyo ni fursa ambayo haipotezwi na wala hairejesheki. Na tawfiiq iko katika mkono wa Allah Subhanahu Wataala .
Na utahadhari usije ukaondoka mahala pako kabla halijatua jua ama baada ya kwisha tua uondoke pamoja na mahujjaji kuelekea Muzdalifah nayo vile vile huitwa Jamaa ukifika hapo useme:
( اللهم إن هذه جمع، فاجمع لي فيها جوامع الخير كله )
Usiwache kufanya talbiya mpaka upige mawe jamrat Al-Aqabah katika siku ya pili, na usisali Al-Maghrib na Al-Ishaa kabla hujafika Jamaa na hivyo ndivyo katika Sunna na ukifika hata lau katika mwisho wa usiku wakati huo ndio usali Al-Maghrib na Al-Ishaa pamoja. Na ulale hapo na umdhukuru Allah Subhanahu Wataala kama ilivyotuelekeza Qurani Tukufu.
البقرة: ١٩٨
“Na mtakaporudi kutoka Arafat mtajeni Allah penye Mash’aril Haraam na mkumbukeni kama alivyokuongozeni.”
Na Mash’aril Haraam ndio Muzdalifah na amesema Allah Subhanahu Wataala :
البقرة: ٢٠٠
“Na mwishapo kuzitimiliza ibada zenu (za Hija), basi mtajeni Allah kama mlivyokuwa mkiwataja wazee wenu; bali mtajeni zaidi (Allah)”.
Waarabu walikuwa wakijifakharisha kwa mababa zao, kwani walikuwa wakiwataja sana basi akawaamrisha Allah Subhanahu Wataala wamtaje yeye badala ya kuwataja mababa zao na hiyo ndiyo kheri kwa mwisho wao (khatima yao).
           
Baada ya kusali Sala ya Al-fajiri hapo Muzdalifa uharakishe kuondoka kuelekea Muna na hapo mashariki ya Muna kuna bonde (wadi) linaloitwa “Wadi Muhassar”. Limeitwa hivyo kwa sababu yule tembo wa Abraha alipokuja kutaka kulivunja Al-Kaaba alishindwa kuendelea asijue pa kwenda akakaa na kila alivyojaribu mwenyewe kumsimamisha ili ende upande wa Al-Kaaba alishindwa na alipokuwa amuelekeza ende upande usiokuwa wa Al-Kaaba alikuwa anakwenda lakini akimuelekeza upande wa Al-Kaaba anakataa kwenda na hukaa chini. Pia huitwa bonde hilo “Wadi Annaar” (bonde la Moto) na lazima anaehiji kulivuka bonde hilo kabla ya kutoka jua siku ya kumi ya Hija.
           
Kitu cha kwanza unachokifanya katika siku hii huko Mina ni kutupa vijiwe kwenye Jamrat Al-Aqaba na vile vile huitwa Jamrat Al-Kubra nalo liko karibu zaidi ya Makka kuliko hizo jamaraat mbili nyingine. Unalitupia vijiwe saba vidogo, ukubwa wake hivyo vijiwe kama kunazi na visipindukie ukubwa huo wala usitupe kisichokuwa jiwe kama wanavyofanya wengi miongoni mwa wajinga watupa viatu au mbao na wayapandia hayo majamaraat na kuyakanyaga kwa miguu yao na kuyapiga kwa mikono yao wengine wayarukia ili wayang’ate, wakiamini kuwa hilo jamarat ndilo shetani na kuwa ati wakimfanyia hivyo huwa wanamdhalilisha. Hawajui masikini kuwa shetani ndiye aliyewapanda wao na kuwa yeye anafurahika na vitendo vyao hivyo kwa sababu ni kinyume na sheria na kinyume na aliyoyaleta Mtume Salallahu Alayhi Wasalam. Na hapa mahala anapopakusudia shetani, Allah amdhililishe na awahidi Waislamu wafanye yanayomridhisha na watende yenye utiifu kwa Mola wao Subhanahu Wataala.
           
Katika masharti ya kutupa hivyo vijiwe ni kuwa ulione hilo jiwe wakati linapopiga hilo Jamarat na upige takbira kwa kila kijiwe unachokitupa useme:
 ( الله أكبر ولله الحمد ، اللهم هذه حصياتي وأنت أحصى لهن مني فتقبلهن مني واجعلهن في الآخرة ذخرا لي وصلى الله على رسوله سيدنا محمد وعلى آله وصحبه وسلم
Baada ya hapa ukiwa ni miongoni mwa wafanyao Hija ya Tamattuu (waliotia Ihram ya Umra kisha wakaitoa na kupumzika na ukawafaa wakati huo wa mapumziko kufanya mambo mengine ya kawaida halafu wakatia Ihram ya Hija ukiwadia wakati wake) utakwenda huko wanakouzwa wanyama ununue mbuzi au kondoo kisha umchinje au ushirikiane na watu sita (muwe jumla saba) mchinje n’gombe au ngamia kwani wanyama wawili hawa watosheleza watu saba. Baada ya hapo unyoe nywele zako au upunguze (ukate nywele) na kunyoa ni bora zaidi kwa mujibu ya hadithi ya Mtume Salallahu Alayhi Wasalam :
( رحم الله المحلقين قيل والمقصرين قال رحم الله المحلقين قيل والمقصرين قال رحم الله المحلقين وفي الرابعة قال والمقصرين )
"Allah amewarehemu wanaonyoa" akaambiwa: Je wanaopunguza akasema "Allah amewarehemu wanaonyoa" akaambiwa: Je wanaopunguza akasema "Allah amewarehemu wanaonyoa" na katika mara ya nne ndio akasema: "na wanaopunguza".
Baada ya hapo unavua nguo zako za Ihram na uvae nguo zako zilizoshonwa na mpaka hapa utakuwa umehalalika mhalaliko mdogo (Tahallul Al-Asghar) na uzidishe kusoma kauli hii:
( الحمد لله رب العالمين رب السموات السبع ورب العرش العظيم وله الكبرياء في السموات والأرض وهو العزيز الحكيم )
Halafu uende Makka ukatufu Al-Kaaba na ufanye Saayi baina ya As-Safa na Al-Marwa kama ulivyofanya wakati ulipofika Makka mara ya kwanza (Al-Quduum) na tawaaf hii huitwa Tawaaf Al-Ifaadhah), nayo ni nguzo ya tatu katika nguzo za Hija na kwa nguzo hii inatimia Hija na hii huitwa mhalaliko mkubwa (Attahallul Al-Akbar).
Iliobakia juu yako sasa ni kurudi Muna ukalale huko usiku wa kuamkia kumi na moja na kumi na mbili kwa wenye haraka na wasiokuwa na haraka walale usiku wa kuamkia tarehe kumi na tatu vile vile. Kulala hapo Muna ni “Sunna Muakaddah” sunna iliyotiliwa nguvu ni lazima ifanywe na atakayeacha kulala lazima achinje na wala wasiseme walio matajiri na wenye kupenda starehe sisi tutalala mahala penye raha halafu tutaziba kosa hilo kwa kuchinja akifanya hivi itakuwa ametoka nje ya sunna na namuogopea kwa kitendo chake hichi kuwa hatokuwa na Hija. Atahadhari.
Katika siku hizi atakazobakia Muna atakuwa kila siku baada ya kupinduka jua (wakati wa adhuhuri) ende kwenye Jamaraat na ayapige kila moja katika hizo Jamaraat tatu vijiwe saba, aanze kwanza Jamarat Assughraa, nayo ndiyo inayofuatia Muna yaani iko mashariki ya zile Jamaraat nyingine kisha apige Jamar Al-Wusta halafu Al-Kubra na zote tatu hizo azipige kutoka kwenye tumbo la wadi (bonde).
Hivi sasa serikali ya Saudia Allah aijazi kheri imepatengeneza hapo mahali kwa kuwajengea sakafu chini na kuwaekea vivuli na mapanka (mafeni). Lakini juu ya hivyo utalijua hilo tumbo la bonde kuwa liko kusini ya hiyo Jamarat Al-Aqaba, na kwa hivyo wakati unapolipiga hilo Jamarat unakuwa umeelekea kasikazini na unaiweka Makka kushotoni mwako. Na hali hiyo hiyo lile Jamarat Assughra lakini Jamarat Al-Wusta inakuwa kinyume ya hivyo, huwa hilo bonde kaskazini yake na ukilitupia mawe huwa unaelekea kusini na unaiwacha Makka kuliani mwako.
Hivyo vijiwe unavyovitupa lazima iwe umeviokota wakati uko katika Ihraam sio wakati umevua hiyo Ihraam. Si lazima kuviokota huko Muzdalifa bali yawezekana kuviokota mahala popote katika Al-Haram hata hapo unapokaa Muna, kwani lazima vijiwe hivyo viwe safi sio kutoka sehemu zenye uchafu kwa sababu hapo wewe unajikaribisha na Allah na haiwezekani kufanya hivyo kwa kitu kilicho kichafu. Ndio maana inapendelewa uvioshe hivyo vijiwe hata vikiwa safi, na inasemwa kufanya hivyo ni katika Sunna.
Jumla ya vijiwe vinavyotupwa sabini kwa mwenye kuchelewa na arubaini na tisa kwa mwenye kufanya haraka. Miongoni mwa wanavyuoni wapendelea kwa mwenye kuharakisha achukue vijiwe ishirini na moja vya nyongeza ambavyo vyampasa mwenye kuchelewa avichukuwe kisha avizike chini ya Jamarat Al-Aqaba. Iwapo litakuchwa jua siku ya kumi na mbili naye bado yupo Muna basi inampasa alale hapo na akae mpaka adhuhuri siku ya kumi na tatu kisha atupe vijiwe ishirini na moja kwenye hizo Jamaraat (kila Jamara moja vijiwe saba).
Kwa kupiga hizi Jamaraat ndio huwa mwisho wa vitendo vya Hija. Hapo umuombe Allah Subhanahu Wataala akukubalie amali zako, wala asikujaalie miongoni mwa waliokhasirika basi ni juu ya mja kufanya jitihada na ni juu ya Allah kupokea vitendo na ni wajibu kwa mja atawakali kwake:
العنكبوت: ٦٩
“Na wale wanaojitahidi kwa ajili yetu, kwa yakini tunawaongoza kwenye njia zetu. Na bila ya shaka Allah yu pamoja na wafanyao mema”.
Ukitaka kuondoka Makka kwa niya ya kutorejea tena katika wakati huu basi inakuwajibikia kutufu tawaaf Al-Wida’a hapo Al-Kaaba. Anayeiwacha tawaaf hii bila ya udhuru basi lazima achinje na haikupasi kufanya saayi baina ya Safa na Al-Marwa.
Kila anayewacha kitendo kimoja katika vitendo vya Hija au ametanguliza kitu badala ya kingine basi lazima achinje mbuzi au kondoo katika ardhi ya Al-Haram, na asiile nyama yake yeye wala aliofuatana nao.
Inapendelewa baada ya Tawaaf Al-Wida’a ende kwenye mlango wa Al-Kaaba na akamate kizingiti chake na aegemeze tumbo lake kwenye ukuta wa Al-Kaaba akiweza kufanya hivyo ama sivyo popote alipo katika Msikiti huo wa Al-Haram aombe Dua ifuatayo:
 ( اللهم لك حججنا وبك آمنا ولك أسلمنا  وعليك توكلنا وبك وثقنا وإياك دعونا فتقبل نسكنا واغفر ذنوبنا واستعملنا لطاعتك اللهم إنا نستودعك ديننا وإيماننا وسرائرنا وخواتم أعمالنا اللهم أقلبنا منقلب المدركين رجاءهم والمحطوطة خطاياهم ، الممحاة إساءتهم المطهرة  قلوبهم منقلب من لا يعصي لك أمرا ولا يحمل وزرا منقلب من عمرت بذكرك لسانه وزكيت بزكاتك نفسه ودمعت من مخافتك عيناه اللهم إني عبدك وابن عبدك وابن أمتك حملتني على دابتك وسيرتني في بلادك وأقدمتني حرمك وأمنك وقد رجوت بحسن ظني أن تكون قد غفرت لي فازدد عني رضى وقربني إليك زلفى اللهم لا تجعل هذا آخر العهد مني عن بيتك الحرام ومن علي بالعودة مرات عديدة وصلى الله على رسوله سيدنا محمد وآله وسلم ) 











4. Usiondoke Muzdalifa kabla ya kusali Al-fajir isipokuwa kwa dharura.
5. Usisali Sala ya Magharibi na Isha isipokuwa baada ya kufika Muzdalifa (kutoka Arafa) hata ikiwa mwisho wa usiku.
6. Usipuuze kuvuka bonde la “Muhassar” (Wadi Muhassar) kabla ya kuchomoza jua.
7. Uhakikishe kuwa vijiwe unavyovitupa vimefika katika hizo sehemu unazozilenga nazo ni Jamaraat.
8. Uhakikishe kuwa unapovitupa vijiwe uvitupe kutoka ndani ya wadi (hilo bonde lilioko hapo).
9. Usichinje kabla ya kutupa vijiwe.
10. Usinyoe kabla ya kuchinja.
11. Usivue nguo za Ihram kabla ya kunyoa.
12. Usiende kutufu Beit Al-Haram(Tawaaf Al-Ifaadha) kabla ya kutupa vijiwe na kuchinja na kunyoa.
13. Uwe na yakini katika tawaf yako kuwa umetufu mizunguko saba. Ukitia shaka basi rudia tena kutufu mpaka uwe na yakini (kuwa umezunguka mara saba).
Hizi zote ni sunna ambazo hamna budi kuzihifadhi au ikiwa hukuzihifadhi utaharibu Hija yako.
Mambo manne yanaharibu Hija moja kwa moja na inambidi anayeyafanya ahiji tena mwaka ufuatiao:
1. Ikiwa hakuhirimia kwa Hija na hakutia niya kutoka mwanzo basi huyo hana Hija.
2. Asiesimama katika Arafa angalau kwa muda wa nusu saa kabla ya kutua jua katika siku ya tisa basi huyo hana Hija.
3. Asietufu Tawaf Al-Ifaadha na kufanya Saayi baina ya As-Safa na Al-Marwa huyo hana Hija.
4. Aliemuingilia mkewe katika hali ya Ihraam au akamchezea mpaka ikamtoka manii basi hana Hija.
Inampasa mwenye Kuhiji aziheshimu amri za Hija na azitukuze kwa mujibu wa kauli yake Subhanahu Wataala:
الحج: ٣٢
“Namna hivi, anayehishimu alama za (Dini ya) Allah, basi hilo ni jambo la katika utawa wa nyoyo.”
Na inampasa mwenye kwenda kuhiji asikithirishe mazungumzo ya Dunia bila ya dharura bali azidishe kumdhukuru Allah na wala asidhulumu, asigombane au kubishana na asighadhibike ghadhabu itakayomsababisha afanye maasi na asubiri katika kila hali inayohitaji subra na hakika Allah yu pamoja na wanaosubiri.











Katika mambo yanayosikitisha sana kuwa baaadhi ya Mahujaji hawataki kuifupisha Sala huko Makka (wakasali zile Sala zenye rakaa nne, kama Adhuhuri, Al-Asiri na Al-Isha, rakaa mbili) kwa madai kuwa mahala hapa ndio asli ya Uislamu na chanzo cha sheria kwa hiyo haisihi kufupisha Sala ndani yake. Na katika kutopea kwao katika ujinga wanatoa fatwa kuwa haifai kusali “Qasran” (kufupisha) basi hatusemi isipokuwa:
إنا لله وإنا إليه راجعون  . Tunawaambia watu: Je Waislamu wamechukua Dini yao kutoka kwa nani? Sio kutoka kwa Mtume Muhammad Salallahu Alayhi Wasalam na yeye ndiye atoaye sheria na hana haki mtu yoyote mwingine kufanya hivyo isipokuwa yeye hata akiwa na cheo kikubwa vipi. Mtume Salallahu Alayhi Wasalam alipokwenda Makka na ndipo alipozaliwa na watani wake wa mwanzo na watani wa baba zake, alipokwenda huko baada ya kuchukua Madina watani wake, alifupisha Sala (za rakaa nne akazisali rakaa mbili) akasema Salallahu Alayhi Wasalam:  أتموا فإنا قوم سفر   Timizeni Sala kwani sisi ni wasafiri.
Jambo hili wamekubaliana nalo Umma wa Kiislamu bila ya kupingana juu yake kwa hiyo hoja gani aliyo nayo yule anayesali Sala kamili bali anapinga kufupisha Sala hapo Makka. Kama ingekuwa kutimiza Sala inaruhusiwa basi wa kwanza aliye na haki hiyo ni Mtume Muhammad Salallahu Alayhi Wasalam kwa sababu yeye kazaliwa hapo na kama alivyosema mwenyewe kuwa katika nchi za Allah anazozipenda kuliko zote ni hiyo Makka na yeye ndiye aliyetuletea sheria ya Allah Subhanahu Wataala. Basi fikirini sana enyi mnaotimiza Sala hapo Makka ima mtakuwa nyie vile vile mmeleta sharia kama alivyoleta yeye Salallahu Alayhi Wasalam basi imebakia kudai Utume na kuwa nyie Mitume au awe Mtume ameficha kitu katika wahyi, na katika jumla ya aliyoficha jambo hili la kufupisha Sala lakini nyie mkaweza kuligundua. Basi mcheni Allah na jihurumieni nafsi zenu, msiende kinyume cha sharia na hali mnadai kuwa nyie ndio mlio katika haki na waulizeni wenye elimu msiharibu amali zenu (vitendo vyenu). Ewe unaetaka radhi ya Allah muendee katika njia yake (aliyoileta) ama sivyo utanyimwa hicho unachokitaka (radhi yake Subhanahu Wataala).











Leo wamekuwa watu wa Dunia nzima majirani wa Beit Al-Haram watu wa Japan katika mashariki, na watu wa kusini ya Canada katika magharibi, na watu wa visiwa vya Siberia katika kaskazini mashariki, na watu wa visiwa vya Hawaii katika kusini magharibi, wote waweza kufika Makka siku hiyo hiyo wanaondoka kwao na wao wako mbali sana na Makka. Ama watu wa Oman anaweza mtu kusali Oman Sala ya Adhuhuri na Sala ya Al-asiri akasali Makka Al-Mukarramah akisafiri kwa ndege.
Ama kwa njia ya bara mtu anaweza kufika Makka katika muda wa saa arubaini bila ya juhudi wala kujikalifisha na njia ina usalama Al-Hamdulillah. Na vyakula na vinywaji na vinavyohifadhiwa katika mafridge na mafreezer vimejaa njia nzima, cho chote mtu anachokitaka zaidi huwa chapatikana. Na wakati huu ndio ule aliokuwa akiutamani Imam “Qeiyd Al-ardh” Allah amrehemu kwani katika niya yake ilikuwa amjaaliye kila mtu anaekwenda kuhiji kutoka Oman asichukue chakula (cha njiani, yaani ajaalie kila kitu kipatikane njiani).
Walikuwa Mahujjaji wachukua kutoka Dhil Huleifa kwenda Makka siku nane na hakuna kinachowazuia na mwangaza wa jua wala na baridi wala na mvua na wao wako katika Ihraam. Leo anapanda mtu gari yenye Air Conditioner katika muda wa masaa manne kutoka Madina mpaka Makka au kwa ndege muda wa nusu saa mpaka Jiddah.
Ilikuwa sehemu wanapotufu watu (kuzunguka Al-Kaaba) wadi chini ya Al-Kaaba hawezi anaezunguka kunyanyua uso wake kutokana na ardhi kwani akifanya hivyo atajikwaa na mawe na mavi ya wanyama na mikojo yao waliokuwa wakiwatumia kutufu juu yake. Leo kama ulivyoona au ulivyosikia ardhi ya eneo hilo linalozungukwa ni safi zaidi kuliko jicho la jogoo wala hamna mteremko wala mlima.
Ilikuwa sehemu inayofanyiwa saayi baina ya Assafaa na Al-Marwa imezongwa na maduka haizidi upana wake mita tano watu wasukumana ndani yake, wakati unapofanya saayi mara wajiona umesukumwa na umerudishwa nyuma mita ishirini. Leo sehemu hii imefanywa njia mbili ya kwenda mbali na ya kurudi mbali na kila njia upana wake mita tano na katikati baina ya njia mbili hizi kuna njia ya kupitishia vigari vya wazee na wasiojiweza. Vile vile kumetiwa ma Air Conditioner (yaburudishayo) na mataa yaangazayo vizuri na juu ya sehemu hii kumejengwa sehemu nyingine ya kufanya saayi isipokuwa mimi binafsi sipendi kufanya saayi huko.
Na alikuwa anaekwenda kusimama Arafah anabeba chakula chake na maji yake juu ya mgongo wake na hubeba kiriba cha maji kutoka Makka mpaka Muna na kutoka Muna mpaka Arafah, na huenda akakosa maji siku nzima kwani ni katika vitu vilivyokuwa shida kupatikana. Leo kila utakapokwenda unayapata maji kwa wingi bali maduka yako kila mahala na hukosi unachokitaka ndani yake.
Ilikuwa kupiga vijiwe “Jamaraat” kazi ngumu sana kwani njia za kukufikisha huko zilikuwa finyu na hazikutengenezwa na ulikuwa msongamano wa watu mkubwa sana, na ilikuwa mtu hafiki huko ila baada ya mashaka makubwa. Leo njia zimepanuliwa na zimesawazishwa na zimetiwa lami na kufika Jamaraat leo ni wepesi sana na vile vile zimeezekwa sakafu hizo njia ili kufanya kivuli na zimetiwa mafeni. Vile vile juu ya sakafu kumefanywa sehemu nyingine ya kurusha mawe lakini mimi sipendi kurusha kutoka huko. Basi tizama neema za Allah Subhanahu Wataala zilizo kubwa za kutusahilishia vitendo hivi vya Hija, na sasa watu wanakwenda kwa wingi sana, zile tabu za mwanzo zimeondoka lakini imekuja tabu ya wingi wa Mahujaji na msongamano kila mahala. Juu ya wingi wa Mahujaji unakuta labda asili mia tano waliokuwa katika njia nzuri ya uongofu kama ilivyosemwa: “Wapandaji (ngamia) ni wengi na Mahujaji ni kidogo”.
Katika athari kuwa mwaka aliohiji Mtume Salallahu Alayhi Wasalam wamehiji pamoja naye watu laki moja (100,000) na katika wakati wetu wa sasa wanaohiji hawapungui milioni mbili 2,000,000, na katika hao asili mia tano 5% kwa wingi kabisa ambao ndio Mahujaji wa kweli kwa mujibu ya hukumu yetu ya dhahiri, na Allah ndie mwenye kujua hakika. Na hiyo idadi ya Mahujaji wa kweli inawafikiana na idadi ya waliohiji pamoja na Mtume Salallahu Alayhi Wasalam. Na imepatikana katika athari: “Ikiwa idadi ya Mahujaji haifiki laki moja basi Allah Subhanahu Wataala anaikamilisha idadi hiyo (laki moja) kwa Malaika”. Yakasihi maneno haya basi yamesihi yale niliyoyakusudia (katika paragraph hii). Na Allah ni mwenye kutoa tawfiiq na kuwaepusha na makosa waja wake, na yeye ndiye anayepokea na kukubali kidogo na kusamehe kingi na yeye ni Mwingi wa Rehema.
Leo unaona maasi wazi wazi chini ya Al-Kaaba hata angalau ile kuihishimu (hiyo Al-Kaaba) ikiwa hawaihishimu Dini yao na Mola wao. Inasemekana kuwa katika zama za mwanzo alimtizama mwanamme mwanamke katika tawaaf basi yakapofuka macho yake basi wasidanganyike wafanyao maasi hapo wakiona haiwashukii adhabu ya Allah haraka:
آل عمران: ١٧٨
“Wala wasidhani wale wanaokufuru kwamba huu muda tunaowapa (wanaishi kwa starehe) ni bora kwao. Hakika tunawapa muda na inatokeya ya kuwa wanazidi madhambi katika muda huo. Na itakuwa kwao adhabu ya kuwadhalilisha.”











Akasema yule mtu mwema: Basi alipomaliza kusema ile Dua sikumuona tena, nikauliza juu yake nikaambiwa yule ni Al-Khadhr AS na nikaihifadhi hiyo Dua. Twamuomba Allah atupe mwisho mwema na atufishe katika hali ya uongofu (hali ya Uislamu).
Tanabahisho:
“Tahiyatul Masjid” ya Msikiti mtukufu huu wa Beit Al-Haram  ni “tawaaf”yaani kuizunguka Al-Kaaba. Anaeingia msikiti huu kitu cha mwanzo anachokifanya ni kuzunguka Al-Kaaba na hiyo ndiyo “Tahiyyatul Masjid” (maamkio) ya msikiti huwo kinyume na misikiti mingine kwani maamkio yake ni Sala. Katika vitendo vilivyo bora sana kuvifanya ni kutufu khasa kwa wanaotoka mbali. Inasemwa kuwa Mtume Salallahu Alayhi Wasalam kasema:
 ( إن لله كل يوم مائة وعشرين نظرة ستون منها للطائفين وأربعون للمصلين وعشرون للناظرين )
 “Hakika Allah anatazama kila siku mitazamo(ya Rehma) mia na ishirini miongoni mwa hiyo sitini ni ya wanaotufu na arubaini ni ya wanaosali na ishirini ni ya wanaotazama” (Al-Kaaba). Basi inataka kuitumia fursa hii kwani ni fursa ambayo haina badili.

No comments:

Post a Comment

Note: only a member of this blog may post a comment.