Tuesday, 19 January 2016

Jezuu 10 Ahli Al-haq na Istiqama ----Kujenga uongofu katika nyoyo za vijana






                  الحج: ٤١

“Wale ambao tukiwamakinisha (tukiwaweka uzuri) katika ardhi husimamisha  Sala na wakatoa Zaka na wakaamrisha yaliyo mema na wakakataza yalio mabaya.

Na marejeo ya mambo ni kwa Allah”

Aya 41 sura ya Al-Hajj


Utangulizi


Shukrani zote anastahiki Allah Subhanahu Wataala, Mola wa walimwengu wote na Rehma zake na Amani zake zimwendee Mtume wake Muhammed bin Abdillah bora wa Viumbe na Mitume. Basi kama ilivyotangulia hii jezuu ya kumi inaendelea kuwa katika mtiririko wa “kujenga Uongofu katika nyoyo za vijana” na tumechagua izungumzie jambo muhimu katika tarehe nalo ni “fikra kwa ufupi juu ya Maimamu wa waislamu katika Omani na nchi nyenginezo iliyoenea ndani yake madhehebu hii “ya Ahli Al-haq na Istiqama”. Amesema Allah SUBHANAHU WATAALA :


يوسف: ١١١

“Bila shaka katika hadithi zao hizo limo zingatio kwa wenye akili”


Na naapa kuwa visa hivyo ni fundisho kubwa kwa anaye refusha fikira na maoni kwani nidhamu ya Uimamu katika Omani imekuja kuwa nguzo ya kimsingi ya kuhifadhi Dini hii tukufu na kuieneza na kuikita mizizi yake.


Ijapokuwa pana tofauti baina ya majina mawili “Uimamu” na “Ukhalifa” isipokuwa yanaonesha kitu kimoja (maana yake ni moja) kwani nidhamu ya “Uimamu” imesimama juu ya msingi wa “Asshuraa” (kushauriana baina ya waislamu) na dalili yake kuwa Imam hapati sharia ya kuhukumu na kuwa Khalifa juu ya rayia isipokuwa baada ya kuchaguliwa (Siyo kwa urithi).


Amesema Sheikh Noor Addiin Assaalmiy -Allah Amrehemu- katika “Madaarij Al-Kamaal”:

“Ni wajibu wamchague Imam wakipata uwezo timamu nao ni kupatikana watu arubaini ambao hawakushughulishwa na baadhi ya mambo kama utumwa, umaskini maradhi na hawakuhitilafiana, lao moja na kati yao wapatikane watu sita wenye elimu (wanavyuoni), na wajiepushe na mambo ya haramu na shubuha, wenye kutegemewa katika elimu na uaminifu na wenye hima kubwa. Wametaraji ushindi katika kusimamisha Uimamu ndio wakaona wamchague aliye bora wao ili awaongoze”


Na katika kitabu “Muqadimat Attawhiid” na sherehe yake kilichotungwa na Mwanachuoni Abi Hafs Amru bin Jamii kuna maelezo juu ya “Uimamu” ambao ameuita kwa jina la “Masaalik Addiin” yaani njia za Dini na idadi yake ni nne:-

1)      Adh-dhuhuur – Uimamu wa kudhihiri.

2)      Ad-difaa’ – Uimamu wa kujihami (na adui).

3)      Ash-shiraa – Uimamu wa kujitolea mhanga.

4)      Al-Kitmaan – Uimamu wa kificho.


Amma Adh-dhuhuur huu ni kama wa Abi Bakar Assiddiq na Omar bin Al-Khattab R.A. na Ad-difaa’ ni kama wa Abdillah bin Wahab Arrasbiy. Na Ash-shiraa’ ni kama Uimamu wa Abi Bilal Mirdaas bin Judere. Na Al-Kitmaan kama wa Abi Ubaidah bin Abi Karimah na Abi Al-Sshaathaa Jabir bin Zeyd R.A.


Kwani hiyo ni wazi kuwa “Uimamu” unatafautiana njia yake ya hukumu kutokana na hali ya mambo iliyouzunguka Umma wa Kiislamu na unawajibika kuchagua msingi wa vitendo unaokabiliana nao.


Bila ya shaka mazungumzo ya “Uimamu” hakiwezi kitabu cha muhtasari (ufupi) kama hichi kuchukua yote yanayohusikana nao isipokuwa lengo ni kuwajulisha Maimamu muhimu na vipi wameeneza daawa yao na Allah ndio pekee mwenye kukusudia kitu kikiwa na yeye ndie Anaeongoza katika njia iliyonyooka.


Imetolewa kuwa Mtume Mohammed -rehema za Allah na amani zimshukie- amesema:

 "يحمل هذا الدين من كل خلف عدوله ينفون عنه تحريف الغالين وانتحال المبطلين وتأويل الجاهلين..."

“Wanaikamata Dini hii waadilifu miongoni mwa wafuatiao (kutoka kwa waliotanguliya) waihami kutokana na upotofu wa wanaopindukia mipaka, na uongo wa wanaojidai wameshika Dini na tafsiri ya wajinga…”


Basi kama hivyo waadilifu wa Ibadhi wameichukua Dini hii na wakasimama katika haki yake kama inavyowajibika, anaichukua afuatiaye kutokana na atanguliaye, na akataae hayo basi akatae au akiri kwani haidhuru kitu mwenye kukataa wala haizidishii kitu mwenye kukiri. Kwa hivyo waadilifu wa kila Karne wameichukua Dini hii kutoka kwa waadilifu wa Karne iliyo kabla yao mpaka wakafikia kwa Mtume wa Allah -rehema za Allah na amani zimshukie- ambaye ndiye chanzo cha asili ya dini hii na ndiye Rehema ya Umma huu naye kaichukua kwa Jibriil Mwaminifu A.S kutoka Allouh Al-Mahfoodh” kutoka kwa Mola Mwenye Nguvu Muabudiwa wa Viumbe na inawatosha Maibadhi sharafu kubwa kuwa wanayo hii Sanadi tukufu (upokezi) haitilii shaka yeyote mwenye akili. Twamuomba Allah Subhanahu Wataala atukinge na upotofu.


Na kama ilivyo hivi sasa tuko katika Karne ya kumi na tano (Hijiri) na wamo ndani yake wanavyuoni wanaojulikana na mkubwa wao Mwanachuoni Mkubwa mujtahid Ahmed bin Hamad bin Suleiman Al-Khaliliy ambaye amewaita wanavyuoni wa Dunia kuja kufanya mdahalo naye (debate) katika maudhuu ya “Al-Aqida” na hakuna aliyeweza kunyanyua kichwa chake kumjibu, Allah Subhanahu Wataala ambariki yeye pamoja na ndugu zake wanavyuoni, wazee kwa vijana.


Basi hao wamechukuwa dini yao kwa waadilifu wa karne ya kumi na nne na wao ni Noor Ad-diin Abdullah bin Hameid As-Saalmiy, na Muhaqiq Amour bin Khamis Al-Maalkiy, Imam wa Waislamu Mohammed bin Abdallah Al-Khaliliy, Imam na Mwanachuoni Mkubwa Majid bin Khamis Al-Abriy, sheikh wa kuaminika Abdullah bin Mohammed Arriyaamiy, sheikh Esa bin Saleh Al-Harthiy na wengineo.


Hao wamechukuwa dini yao kwa waadilifu wa karne ya kumi na tatu na hao ni: sheikh Arrabani Saeed bin Khalfan Al-Khaliliy na sheikh Saleh bin Ali Al-Harthiy, Mohammed bin Salim Al-Ghaarbiy, Nasser bin Jaaiid Al-Kharusiy na Sultan bin Mohammed Al-Battashiy na wengineo.


Na hao wamechukuwa dini yao kwa waadilifu wa karne ya kumi na mbili na hao ni: sheikh Saeed bin Bashiir Assubhiy, sheikh Jaaid bin Khamis Al-Kharusiy, sheikh Saeed bin Ahmed Al-Kindiy, sheikh Khalaf bin Sinan Al-Ghaafriy, sheikh Nasser bin Suleiman na Mohammed bin Midaad.

Na hao wamechukuwa dini yao kwa waadilifu wa karne ya kumi na mmoja na hao ni: Sheikh Khamiis bin Saeed Asshaqsiy, sheikh Masood bin Ramadhan Annabhaniy, shiekh Khamiis bin Ruweishid Al-Majrafiy, Sheikh Saleh bin Saeed Al-Zaamily na Sheikh Abdallah bin Mohammed bin Ghassan Al-Kindiy.


Na hao wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya kumi nao ni Mohammed bin Abdulbaqiy mwanachuoni mkubwa kabisa na sheikh Abdallah bin Omar bin Ziyad Al-Shaqsiy na Mohammed bin Ahmed bin Ghasan na mwanachuoni mkubwa Ahmed bin Midaad na sheikh Mohammed bin Abdallah bin Midaad . Na hao wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya tisa nao ni Ali bin Abdulbaqiy na Sheikh Ahmed bin Saleh bin Mufarraj na sheikh Saleh bin Wadhaah, na Sheikh Suleiman bin Ahmed bin Mufarraj na Sheikh Abu Alhassan bin Khamis bin Amour. Nao wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya nane nao ni Mwanachouni mkubwa Saeed bin Ahmed bin Mohammed bin Saleh, na Sheikh Abu Al-Qassim bin Abu Shaaeq na ndugu yake Abdul Al-Rahman bin Abu Shaaeq, na Shekh Suleiman bin Rashid bin Saqr Al-Adawiy na ndugu yake sheikh Dahman bin Rashid bin Saqr basi hao wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya saba nao: Ahmed bin Al-Nadhr bin Suleiman mwanachuoni aliekufa shahidi na aliuliwa  na Khardala Al-Jabbar, na sheikh mkubwa Abu Omar Al-Nakhliy, na sheikh Saeed bin Ahmed bin Mahmood , na Abu Al-Miikaal Musa bin Kahlaan , na sheikh Abu Othman bin Abu Abdallah  ajulikanae kwa " Al-Assam" Allah Subhanahu Wataala Amrehemu. Hao  wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya sita nao ni mwanachuoni mkubwa Al-Khudhr bin Suleiman babu wa Ahmed bin Al-Nadhr alietangulia kutajwa, sheikh Ahmed bin Abdallah bin Musa, na Sheikh Mohammed bin Ibrahim bin Musa na mtoto wa ami yao Mohammed bin Musa Al-Kindiy na Sheikh Abu Mohammed Abdallah bin Mohammed bin Ibrahiim As-Samailiy basi wao wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya tano nao ni mwanachuoni mkubwa Abu Ali Al-Hassan bin Saeed bin Quraysh, na mwanachuoni mkubwa Salama bin Muslim Al-Utabiy As-Sohariy, na mwanachuoni mkubwa Mohammed bin Abdallah bin Al-Mufadda Al-Kindiy, na Al-Qadhiy Abu Abdallah Mohammed bin Essa , na Al-Qadhiy Abu Ali Al-Hassan bin Ahmed Al-Hajaariy na Mwanachuoni mkubwa Abu Al-Hassan Al-Bisyawiy na hao wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya nne nao ni Imam wa madhebu Abu Saeed bin Muhammed bin Saeed Al-Kadamiy Al-Naabiy, na Sheikh Al-usuuliy Abu Muhammed bin Barakah, na Mwanachuoni Mkubwa Abu Muhammed Al-Hawaariy bin Othman na Mwanachuoni Mkubwa Abu Mohammed bin Abdallah bin Mohammed bin Abi Al-Muathir na hao wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya tatu nao ni: Mwanachuoni Mkubwa Musa bin Ali, na Mwanachuoni Mkubwa Mohammed bin Mahboob bin Al-ruheil, na Mwanachuoni Mkubwa Abu Almuathir As-Salt bin Khamis, na Mwanachuoni Mkubwa Abu jaabir Mohammed bin Jaafar, na Mwanachuoni Mkubwa Basheer bin Mohammed bin Mahboob na Mwanachuoni Mkubwa Al-Mualliy bin Muniir na hao wamechukua dini yao kwa waadilifu wa karne ya pili nao ni Al-Rabii bin Habib mwenye kitabu “Al-Musnad As-Sahiih” ndio marejeo ya madhehebu ya Ibadhi katika hadithi .Na wachukuaji wa elimu walioichukua kuipeleka Oman nao ni watano mashuhuri nao ni Mahboob bin Al-Ruheil bin Saif bin Hubeira na Saif babu yake mpiganaji katika wapiganaji wa Mtume wa Allah -rehema za Allah na amani zimshukie, na Al-Munir bin Nayer Al-Jaalaaniy Al-Riyamiy, na Mohammed bin Al-Maaliy Al-Kindiy, na  Bashiir bin Al-Mundhir An-Nizwaniy, na Musa bin Abiy Jabir Al-Azkaaniy na mamia wa wanavyuouni wakubwa kama mfano wa hao waliotajwa : Kahlan bin Attia Qadhi wa Imam Al-Julandiy bin Masood na wale waliokufa mashahidi pamoja na Imam hapo Galfar. Basi ni za Allah hizo nafsi zilizosafika ambazo haziwezi kutiliwa shaka katika ukweli na uikhlasi wake. Allah Azirehemu roho Hizo na Azikirimu kwa kuzipa fadhila zake na daraja kubwa.


Na kadhalika hao wamechukua ilimu yao kutokana na waliowatangulia waliokuwa wenye heshima, waadilifu wa karne ya kwanza ambayo ni bora ya karne zote nao ni: Jabir bin Zayd “Abu As-Shaathaakatika Matabiin wanaotegemeka kabisa rafiki wa Al-Hassan Al-Basriy na Mazin bin Ghudhuba As-Saadiy As-Samailiy naye ndie alichukua habari za bishara njema za Utume wa nabii Muhammed -rehema za Allah na amani zimshukie- kuwafikishia watu wa Oman, na Saif bin Habiira Mpiganaji wa mtume Muhammed -rehema za Allah na amani zimshukie, na Abd na Jeyfar watoto wa Al-Julanda Wafalme wa Oman, na Jaafar bin khathm Al-Atkiy na Abu Safra Saarif bin Dhaalim, na Sohar bin Al-Abbas Al-Abdiy, na Al-Qaadhiy Ka’ab bin Suur. Na wale waliochukua elimu katika karne hii ambao watu wa Oman wamechukua kutoka kwao ni Abu Obaidah Muslim bin Abi Karima Al-Tamimiy, na Abdallah bin Abadh ambaye kutokana naye imepewa jina Madhebu hii ya maridhiya ya “Ibaadhi” na huyu Abdallah bin Abadh ni Imam wa siyasa wa kiibadhi sio Imam wa elimu ndio maana hukuti athari yake yoyote ya kutunga vitabu. Anasema Sheikh wetu Noor Addiin As-Saalmiy, Allah Subhanahu Wataala Amrehemu, katika shairi na yafuatayo ni maana ya hilo shairi:


“Sisi Maibadhi hakutuwekea madhehebu hii mwana wa Ibaadh tuifuate ndio maana hukuti katika vitabu vyetu masala yake hata moja imeandikwa. Basi sisi katika Asili na katika matawi tuko katika njia iliokuwa juu kabisa ya salafu (Masahaba). Kwa hiyo twachukua haki pale tunapoiona hata kama kaileta mtu tunaemchukia na baatili twairudisha hata kama imeletwa na rafiki anaependwa kwetu. Na tunaokhalifiana nao (katika medhebu nyingine) wao ndio waliotwita jina hili la Ibadhi na sisi tumeridhika nalo (hatukulipinga)”.     


Na wa kwanza katika hao waliokwisha kutajwa ambao Maibadhi wamewategemea katika utowaji wa hadithi ni Jabir bin Zayd. Kwa ajili ya uaminifu wake ametegemewa na hatiliwi shaka katika utowaji wake wa habari  na yoyote yule akiwa ni Muibadhi au sio Muibadhi, na wamemsifu wengi katika waliotunga vitabu na kama walivyomhusudu wengi wamejua uadilifu wake lakini juu ya hivyo hawamtaji katika vitabu vyao kama ilivyokuja katika mithali “Twakuona na wewe si chochote”. Na Imam Jabir kama alivyokuwa mashuhuri katika vitabu vya sira kuwa amewawahi (amewakuta) Masahaba Sabini waliopigana katika vita vya “Badr” basi inatutosha kuwa masahaba wengine aliowakuta walikuwa wengi sana. Katika mashekhe wake wakubwa (aliochukua elimu kwao) ni Abdallah bin Abbas na Bibi Aisha Mama wa waumini Radhi za Allah ziwe juu yao. Inasemekana kuwa si chini ya masahaba khamsini alichukuwa elimu kwao baina yao Anas bin Malik, Abu Ayoub, Abu Hurairah na wengineo wengi. Na hapana shaka yoyote kuwa alichukua elimu kutoka kwa Masahaba Radhi za Allah ziwe juu yao yaani amechukua katika chanzo kilichokua safi kabisa bila ya wasiwasi wala shaka yoyote. Basi pima ewe uliokuwa na akili wapi penye haki zaidi kuchukua penye chombo safi kilichokuwa hakikuchafuliwa au penye chombo kilichopita katika mikono mingi na kurambwa na ndimi na kikaingiliwa na wale wenye uwezo wanaofuata mapendekezo ya nafsi zao baada ya kitambo cha wakati? Basi insaaf  (kupima mambo kwa haki) ni tabia ambayo Allah Subhanahu Wataala huipenda kwa hivyo ukitumia Insaaf utaona kile chombo cha kwanza ndicho moyo unapotumaini na nafsi kuridhia. Basi baadhi ya wana historia wasema: “Maibadhi madhehebu yao katika ukweli na uaminifu ni madhehebu ya Abu Bakr Al-Siddiq, na madhehebu yao katika mkazo na uongofu ni madhehebu ya Omar bin Al-Khattab na Akida yao ni Akida ya Mtume wao Muhammed -rehema za Allah na amani zimshukie- hawako tayari kubadili dini yao kwa ajili ya dunia wala hawawafanyii uadui waislamu wala hawajibagui (wawa pamoja nao) na Waislamu na humsifu Allah Subhanahu Wataala kwa sifa zake zilizokamilika na zilizo bainika (zilizokuwa wazi ambazo hazipingani na utukufu wake Subhanahu Wataala). Wamtukuza Allah Subhanahu Wataala na kumyanyua kutokana na kila aina ya upungufu na aibu. Msingi wa dini yao ni kitabu (Qur’ani) na Sunna ya Mtume -rehema za Allah na amani zimshukie- na utegemeo wao kwa vitu hivi viwili ni wenye nguvu kabisa bila ya kulainika kisha vile vile wanategemea Ijmaa na kutenda kwa mujibu wake kisha wachukulia rai katika mambo waliyokhtilafiyana nayo Waislamu na hawamridhii mtu yoyote yule atakapo pinga njia ya Waislamu basi hata akiwa yeye nani au daraja yake iko vipi.


Kuelezea kwa ufupi juu ya Maimamu wa Oman

Hazikufanikiwa madhehebu nyingine za kiislamu kutawala katika msingi wa kitabu (Qur’ani) na Sunna kwa njia ya Makhalifa walioongoka kama walivyofanikiwa Maibadhi. Akitaka mwenye kupenda haki na Insaf basi asome tarekhe na ataona ukweli wa haya tuliyoyasema. Ndio wao wanao watawala wamewaita “Maimamu” basi twamshukuru Allah Subhanahu Wataala kwa mafanikio yake.


1)      Imam Al-Julanda bin Masood bin Muawala bin Shams:

Huyu ni Imam wa kwanza aliochaguliwa Oman katika mwaka 132 H na alikuwa katika wafalme wa Oman baada ya watoto wa Malik bin Fahm na alikuwa amezungukwa na wanavyuoni wakubwa na hautoshi ufupi wa maelezo haya kuwataja hao wanavyuoni, na huyu Imam ametawala muda wa miaka miwili na mwezi mmoja na amekufa shahidi yeye pamoja na maaskari wake elfu kumi wameuliwa na maaskari wa mmwagaji damu wa utawala wa Ki-Abbasi ambaye Allah Subhanahu Wataala kamsaliti na maradhi ya ndui akafa huko Al-Anbar.


2)      Imam Al-Warith bin Kaab Al-Kharusiy naye anatoka Al-Hijaar, Wadi Baniy Kharus:

Siku moja kasikia sauti haijui itokapo wala nani mwenyewe yamwambia asimamishe uadilifu (atawale kwa sharia ya kiislamu kutumia kitabu na Sunna). Basi akachaguliwa na waislamu kutawala na kipindi chake kimechukua miaka kumi na mbili na miezi fulani, kwani alichaguliwa mwaka 179 H na akafa mwaka 192 H na sababu ya kifo chake alizama katika ‘Wadi Kelbuu’ huko Nizwa iliosabibishwa na mvua na vile vile walikufa pamoja na yeye masahibu zake sabini wakati alipoona mkondo wa maji unawaendea wafungwa, kwani jela ilikuwa kando ya wadi, akasema hawa ni amana yangu na mimi nitaulizwa kesho juu yao basi akajitupa katika wadi ili kuwaokoa yakawashinda nguvu maji yeye pamoja na wenzake Rehma za Allah Subhanahu Wataala ziwe juu yake.


3)      Imam Ghassan bin Abdallah Al-Yahmadiy kutoka Al-Fajah:

Amechukua Uimamu baada ya kufa kwa Imam Warith moja kwa moja bila ya kuchelewa katika mwaka 192 H naye ni wa kwanza aliyohami bahari kutokana na maharamia wa bahari wa kihindi waliokuwa wakiwatisha na kuwatia khofu watu katika bahari. Basi akawapelekea askari wake wakawashinda kwa hivyo ikawa ndio mwisho wa uharibifu wao baharini. Jeshi la bahari la Omani liliokuwa na Idadi kubwa ya manuwari lilikaa macho kila linaposikia kuna maharamia baharini linakwenda kuwahujumu na hatimaye wakawafukuza kabisa kutoka pwani ya bahari ya Oman. Katika wakati wa Imam huyu ndipo yalipohamishwa makao makuu ya serikali kutoka Sohar kwenda Nizwa baada ya kukubaliana wanavyuoni waliona maslaha juu ya kitendo hicho. Naye ni wa kwanza aliyekata mkono kwa  kosa la kuiba huko Sohar. Alitawala miaka kumi na tano na miezi saba kwa uadilifu. Aliumwa siku ya Jumatano tarehe 22 Dhil-Qe’edah na akafariki usubuhi wa Jumapili katika mwezi huo huo kabla ya kumalizika mwaka 207H kwa siku nne. Allah Subhanahu Wataala amrehemu.


4)      Imam Abdil Malik bin Humaid katokana na Bani Ali bin Sawda bin Ali bin Omar bin Aamer Al-Alawiy Al-Uzdiy:

Amechaguliwa kuwa Imam mwaka mmoja baada ya kufa aliyomtangulia katika Shawwal mwaka 208 H. amechaguliwa katika msingi ule ule aliyochaguliwa Ghassan na kabla yake Al-Warith na Al-Julanda na kabla yao makhalifa walioongoka na msingi wenyewe ni kuamrishana mema na kukatazana mabaya na kuiuza nafsi kwa ajili ya Allah Subhanahu Wataala na kupigana na waasi wa Imam (yaani waliotoka nje ya utiifu wake). Amesema Imam Noor Ad-diin: “Iligeuka Oman katika wakati wa Imam huyu ikawa bora kuliko nchi zote za Allah Subhanahu Wataala Wakati alipozeeka Imam waislamu wakaigopea nchi yao kupotea basi hapo ndipo alipochukuwa hatuwa Musa bin Ali ambaye ndiye aliyekuwa marejeo ya wanavyuoni wakati huo ya kumsaidia mpaka alipokufa siku ya Ijumaa katika mwezi wa Rajab mwaka 226H Allah Subhanahu Wataala Amrehemu. Ulidumu uimamu wake miaka 18 na siku saba.


5)      Imam Al-Mohanna bin Jeifar Al-Yahmadiy:

Imam mkubwa kuliko maimam wote wa jamii hii ya Al-Yahmad, ukubwa wa dini na dunia. Alikuwa akiitwa mwenye nabu (magego) kwani alikuwa akikasirika hutokeza meno yake na huenda baadhi ya walio karibu yake wakafa kwa heiba yake. Kachaguliwa siku ile ile aliokufa yule Imam aliyomtangulia nayo ni siku ya Ijumaa tarehe 3 mwezi wa Rajab mwaka 226H. Na alikuwa haingii mtu yoyote kwake isipokuwa ana silaha na hakuwa mtu yeyote akizungumza katika majlis yake. Alikuwa amekusanya baina ya nguvu ya bara na ya bahari na ikafikia nguvu hii kiwango kikubwa sana. Zilifika manuwari mia tatu za vita, ngamia mia saba na farasi mia sita. Nguvu hii ilipatikana bila ya kuchelewa katika mwito wa mwanzo wa vita. Alifariki Imam huyu Allah Subhanahu Wataala amrehemu siku ya Ijumaa tarehe 16 mwezi wa Rabii Athaniy mwaka 237H, baada ya kutawala miaka kumi na moja kasoro miezi michache. Na alikufa kabla yake sheikh wa kiislamu Musa bin Ali katika Rabii Al-Awwal mwaka 230H na aliathirika sana Imam kwa kifo chake, Allah Subhanahu Wataala awerehemu wote.


6)      Imam Assalt bin Malik bin Balarab Al-Kharusiy:

Amechaguliwa katika siku ile ile aliyokufa aliyekuwa kabla yake siku ya Ijumaa 16 Rabee Al-Aakher mwaka 237H. Miongoni mwa wanavyuoni wakubwa  waliomchaguwa ni Mohammed bin Mahboob. Katika maimamu wote hakuna aliyeishi muda mrefu zaidi katika utawala kama Imam Assalt, alitawala mpaka akazeeka wakachoka nae raia zake na ukweli athari ya uzee wake ilionyesha katika miguu yake lakini maskio yake, macho yake, akili yake na ulimi wake vyote hivi havikupata upungufu wowote. Imam huyu ndiye yule mwenye ile karama wakati mwanamke fulani huko Socatra alikuwa akiomba msaada kwake akaandika barua kisha akaitia ndani ya kipande cha bomba akakitumbukiza baharini basi ikahifadhika na kwenda masafa marefu katika bahari mpaka ikamfikia Imam huko Sohar. Mwanamke huyu kabila yake ni Jahdhamiy katika watu wa Samad Asshaan, alikuwa huko Socatra wakati lilipotokea lile tukio maarufu katika historia ambalo lilisababisha watu wa Oman kufarikiana katika makundi matatu (rejea siira) akatoka Imam kutoka nyumba ya Uimam katika tarehe 3 Dhil Hijja mwaka 272H baada ya kutawala miaka thalathini na tano na miezi saba.


7)      Imam Rashid bin Annadhar Al-Yahmadiy:

Naye ndiye aliyesimama pamoja na Musa bin Musa na wenzao wengineo kumtoa Imam Assalt kutoka katika Uimamu. Walipomwingilia Imam Assalt akatoka kuiwacha nyumba ya Uimamu bila ya kugoma au kufanya upinzani wowote, baada ya kutoka tu huku nyuma wakafanya uchaguzi wa Imam mwingine na ndio alipochaguliwa huyu Imam Rashid na ilikuwa katika siku ya Alkhamiis tarehe 3 Dhil Hijja mwaka 272H. na katika kipindi chake hichi cha utawala kulitokea fitna nyingi sana na wakauliwa watu wengi sana hata mwisho ikabidi waivamie nyumba ya Uimamu  wakamkamata na kumtoa humo baada ya kupita miaka minne na siku khamsini na nane katika utawala na wengi katika watu wa Oman walikuwa hawako radhi nae na kukhitilafiana kulikuwa kwingi sana Allah Subhanahu Wataala pekee anajua ukweli na haki iko wapi. Na kwa sababu ya fitna hizi wakagawanyika watu wa Oman makundi mawili. Kundi la Nizwaniyah likiongozwa na Imam Abu Saeed Al-Kadamiy na Kundi la Rustaqiyah likiongozwa na Imam Abu Mohammed ibn Barakah na juu ya tukiyo hili ametunga Imam Abu Saeed kitab “Al-Istiqamah”.


8)      Imam Azzan bin Tameem Al-Kharusiy:

Amechaguliwa kuwa Imam siku ya Jumatano tarehe 3 mwezi wa Safar mwaka 277H. na katika wakati alipotawala vimetokea vita vingi vya kupigana Wa-Omani wenyewe kwa wenyewe. Katika hivi ni vile vita vya Izki ambavyo aliuliwa Musa bin Musa na vile vile vita vya Alqaa katika Sohar ambavyo waliuliwa wengi katika watu mashuhuri Oman. Na asili ya vita hivi vyote ni watu wa “Jarnan” mpaka ikawa inasemwa (Haitokei fitna Oman isipokuwa asili yake ni Jarnan) .Na vikasababisha vita kuingiza shari Oman na watu kukimbia kwenda Bahrain na huko kuna yule mtu anaeitwa Mohammed bin Noor (wakaipindua watu wa Omani badala ya Noor wakamwita Boor). Wakaweza kumchota kwa maneno yao matamu na akawakubalia kuwasaidia hapo akenda na jeshi lake Oman lililokuwa na wapiganaji 25,000 na farasi 3,000 na akaleta uharibifu mkubwa Oman kwani aliua maelfu na kufukia mito ya maji, akaunguza vitabu, akakata mikono, akasababisha masikio yapate uziwi na macho yapate upofu, mwishowe akauliwa Imam Azzan bin Tameem huko Samad As-Shaan mwaka 270H. ukawa umedumu Uimamu wake miaka mitatu.


Baada ya Imam Azzan wakateuliwa Oman maimam wanane ambao haikujulikana vizuri tarehe yao baadhi yao wamejiuzulu wenyewe na baadhi yao wametolewa na wengine wameuliwa na kadhalika ikaendelea hali hiyo ya kivita Oman na kutokuwa na utulivu mpaka Allah Subhanahu Wataala aliekuwa kareem akaleta neema yake kwa kumleta:


17) Imam Saeed bin Abdallah bi Mohammed bin Mahboob Al-Ruheiliy Al-Qurashiy:

Na familiya hii ya Al-Ruheiliy ilikuwa na mahala pakubwa baina ya wanavyouni wa Kiislamu. Familia iliyobarikiwa inafuatia Istiqama kutoka kwa waliopita nyuma (wazee) kwenda kwa vizazi vyao na babu yao ni Seif bin Hubeira mpiganaji wa Mtume Mohammed -rehema za Allah na amani zimshukie- na kuchaguliwa kwa Imam Saeed kulikuwa katika mwaka 320H. naye ni katika wale waliokubaliana waislamu katika Uimamu wake na kutawala kwake kwani hakuna aliempinga au kumtolea kasoro yoyote ile hata wakasema baadhi ya wanavyuoni wa siku zake kuwa hatujui imamu yoyote katika maimamu wa waislamu waliotawala hapa Oman aliekuwa bora kuliko Saeed bin Abdallah isipokuwa  Al-Julanda bin Masood.


Amesema Imam Noor Ad-diin: “Simweki sawa Imam yoyote Oman na Imam Al-Julanda kwani yeye amejumuisha sifa tatu nazo ni elimu, uadilifu na shahada (kufa shaheed). Na kwa Imam huyu (Saeed bin Abdallah) Allah Subhanahu Wataala amemdhalilisha Yousuf bin Wajeeh na wasaidizi wake wa dola ya Al-Abassiya nao ndio waliobakia katika askari wa Ibn Boor basi wakatoka Oman hali ni dhalil na wala waislamu hawakuhalalisha kitu katika mali zao wakati wa kufukuzwa kwao hata pete ya reza ya mlango ilipotea basi Imam akawaadhibu wale walioichukua na wakairudisha kwa wenyewe. Tizama huu uzuri na ukarimu kwa ajili ya Allah Subhanahu Wataala” Alikufa Imam shaheed katika mwaka 328H. na ulikuwa Uimamu wake miaka minane rehema na ridha za Allah Subhanahu Wataala ziwe juu yake.


18) Imam Rashid bin Al-waleed Al-Kindiy:

Alikuwa katika upande wenye nguvu wa uchaji Mungu na mahala pa juu pa uongofu. Amemsifu Imam Abu Saeed huyu Imam Rashid kwa sifa nzuri na za ajabu. Amesema Imam Noor Ad-diin : Inakutosha kujua hali nzuri ya yule mtu anaesifiwa na Abu Saeed sifa kama hizi. Na watu ni mashahidi wa Allah Subhanahu Wataala katika ardhi yake. Kisha akawaingilia fattan wa Iraq na jeshi lake kubwa akaiteka Oman kwa msaada wa watu wake na kwa ubaya wao kwa Imam wao basi akajitenga Imam kwenda mahala palipo magharibi ya Jabal Akhdhar, akaishi huko kama alivyojaliwa kuishi mpaka kufa kwake naye yu katika hali ya kusifiwa. Tarehe ya kufa kwake haijulikani isipokuwa imeandikwa katika “Bayaan Asshara” kuwa Oman iligeuka kuwa nchi ya Ukafiri na Unafik katika mwaka 342H na wakti huu ndio hapo ilipotekwa Oman. Msaada wote ni kutoka kwake Allah Subhanahu Wataala Amesema Sheikh Salim bin Hmood Assiyabiy: “Imepita karne hii nayo Imetandwa na mawingu ya dhulma na ufisadi kutokana na hawa wasaliti wa Bani Abbas juu ya Umma wa kiislamu na walikuwa kama waliowatangulia yaani Bani Umayya balaa na shari kubwa kwa Umma wa kiislamu. Allah Subhanahu Wataala ndio mtoshelezaji wao na wetu (waislamu).


19) Imam Al-Khalil bin Shadhaan bin Salt bin Malik Al-Khrusiy:

Kwake ndio limenasibishwa kabila la Al-Khaliliy katika Oman nalo ni kabila muhimu sana katika Oman, mtiririko unaofatana kama mtiririko wa kabila la Ar-Ruheiliy. Ilibakia Oman na watu wake yachezewa na watu majabari mpaka Allah Subhanahu Wataala akajalia kuja huyu Imam Al-Khalil ambaye alichaguliwa kuongoza katika mwaka 444H. akenda baina yao mwendo mzuri na kuwalinda kutokana na majabari na kwa uadilifu wake ikawa amani katika nchi na wakastarehe katika utawala wake waja. Alifikiwa na Imam Abu Is-haq Al-Hadhramiy kutoka Hadhramaut kwa kumuomba msaada amsaidie kupigana na watu wa Yemen na Hadhramaut katika wale waliotoka katika utiifu wake basi akamsaidia kwa mali na watu mpaka akaweza kuweka Imara nguzo za uimamu na akamsifu Imam Abu Is-haq Imam Al-Khalil katika kasida zake zilizomo katika Diwani yake maarufu. Yakatokea mambo makubwa katika wakati wake pamoja na kuhujumiwa na maadui lakini alifanikiwa kuwashinda na kuleta hali nzuri mpaka Allah Subhanahu Wataala alipomchukuwa katika rehma yake na radhi zake katika mwaka 462H baada ya kuongoza miaka 18.


20) Imam Rashid bin Saeed Al-Yahmadiy:

Amechaguliwa kuwa Imam baada ya Imam Al-Khalil naye vile vile amemsaidia Imam Al-Hadhramiy (Imam wa Yemen na Hadhramaut) kwa mali na kwa watu kama alivyofanya aliyekuwa kabla yake Imam Al-Khalil. Na ameandika (Imam Al-Hadhramiy) juu yake (Imam Rashid) kasida za kumsifu katika diwani yake. Akawakusanya wanavyuoni katika wakati wake wakaweka kikomo cha mushkila wa Assalt na Musa na hapo ndipo walipokubaliana kuwa yeyote aliesikia juu ya kosa lililofanyika na kumjua alietenda hilo kosa ni juu yake kumkata au kuachana naye (kumchukia kwa ajili ya Allah Subhanahu Wataala na kutomwombea Rehema na Maghufira) na ikiwa haelewi hukumu ya kosa hilo juu yake kuuliza na  akishaeleweshwa hukumu yake basi ni wajibu wake kumkata huyo mkosa na anayetilia shaka hukumu hiyo huyo amehiliki. Akabakia Imam huyu maridhiwa hata kufa kwake huko Nizwa. Rehma za Allah Subhanahu Wataala juu yake.


21) Imam Hafs bin Rashid bin Saeed Al-Yahmadiy:

Alibakia katika uimamu muda mrefu lakini haikupatikana tarekhe yake kujulikana lini amechaguliwa na lini amekufa. Kila ajali imeandikwa na Allah Subhanahu Wataala.


22) Imam Rashid bin Aliy Al-Kharusiy.

Amesema Imam Noor Ad-Diin: “Hatukupata kujua tarehe ya kuchaguliwa kwake lakini kinachojulikana kuwa alikuwa Imam mwema wamemshukuru raia zake na umma wa Kiislamu kumhimidi kwani alikuwa mnara wa uadilifu na amekufa mwaka 513H.


23) Imam Amir bin Rashid bin Al-Waleed Al-Kharusiy:

Alikuwa mtu mwenye elimu na alikuwa zaahid (hakuchukuwa katika dunia isipokuwa cha dharura) mwenye akili na maarifa anawatendea mema raia zake na alikuwa Imam aliyeuza Dunia yake kwa ajili ya Allah Subhanahu Wataala (Imam As-Shari) naye ni katika maimamu wa Bani Kharus wa As-Shari wa mwisho na akasimamiya haki mpaka mwisho wake. Rehema za Allah Subhanahu Wataala ziwe juu yake. Amechaguliwa kuwa Imam  katika mwaka 576H. Wakati wa kufa kwake haukuhifadhiwa wala wa kubakia kwake katika uimamu kama ilivyokuwa haikuhifadhiwa tarehe ya Imam wa kumi na tano Mohammed bin Ghassan bin Abdallah Al-Kharusiy na alikuwa Imam wa difaa na alikuwa katika uimamu wake muadilifu hakumkosoa kitu mtu yeyote katika wakati wake wala kupinga katika hukumu zake mpaka Allah Subhanahu Wataala kumchukuwa kwake. Rehema za Mola Subhanahu Wataala ziwe juu yake.


24) Imam Al-Khalil bin Abdallah bin Omar Al-Khaliliy:

Katika watoto wa Salt bin Malik na hakutolewa makosa katika uwongozi wake mpaka Allah Subhanahu Wataala akamfisha naye yu hali ya kunyooka katika njia ya haki. Naye ni katika maimamu waliokuwa tarehe zao hazijulikani. Utawala wa kiabbasi ulikwisha kwa kumalizika karne ya sita Hijri na hapo ndio ilipotoweka dola yao na ikapumzika ardhi kutokana nao na wala mbingu haikuwalilia (kwa mambo yao yalivyokuwa mabaya). Oman nayo ikapumua kwa kupumzika na dhulma zao. Sifa zote na shukrani azistahiki Allah Subhanahu Wataala Lakini kwa ajili ya maovu ya wale watu wabaya wa Oman na kupigana kwao wenyewe kwa weneywe na kugawanyika, Allah Subhanahu Wataala akawasaliti juu yao madhalimu wengine kutokana na wao wenyewe wakawaonjesha adhabu iumizayo kwani kama vile mlivyo ndivyo mnavyotawaliwa. Tazama hikma ya Mola Subhanahu Wataala kwani Bani Abbas walitawala muda wa miaka mia tano kesha wakadhalilishwa na Mwenyezi Mungu Subhanahu Wataala baada yake. Kama ilivyokuja zamu ya Al-Yaariba baada ya miaka mia tano mingine wakawan’goa majabari kutokana na dhulma yao wakaijaza Oman uadilifu kama ilivyokuwa imejazwa udhalimu na katika kipindi hichi akachaguliwa Imam:


25) Imam Al-Hawari bin Malik.

Amechaguliwa mwaka 809H na akasimama katika wajibu wa sharia na akafanya kwa uwezo wa nafsi yake kuleta uadilifu. Alifariki mwaka 833H baada ya kutawala kwa miaka ishirini na tatu. Na wakamchagua:-


26) Imam Malik bin Al-Hawari.

Alikuwa mwenye kushukuriwa kwa mwendo wake mzuri lakini hakudumu zaidi ya mwaka mmoja katika uimamu wake kisha akachaguliwa Imam:-


27) Abu Al-Hassan bin Khamis bin Aamer:

Katika mwezi wa Ramadhani mwaka 839H. na akadumu katika uimamu mwaka mmoja basi kisha Allah Subhanahu Wataala akaleta kwa fadhli zake mtu shujaa mwenye nguvu akawa imara mbele ya watu waovu. Na huyo ni:



28) Imam Omar bin Al-Khattab:

Namna alivyowahujumu madhalimu mfano wake ni kama Simba anaehujumu, basi Allah Subhanahu Wataala akampa ushindi juu yao na akamrithisha ardhi yao na nyumba zao akatoa amri zichukuliwe mali zao na Bait al Maal. Amechaguliwa Imam mwaka 885H kisha wakatawala kiasi maimam watano katika kipindi hichi lakini walikuwa madhaifu na wakaonewa na watu majabari mpaka alipokuja kutawala mtu mwenye ushujaa na uadilifu:


29) Imam Mohammed bin Ismaeel Al-Haadhriy:

Ametokana na Qudhaa bin Malik bin Himyar. Allah Subhanahu Wataala kaujaza moyo wake Imani na akautia nguvu na akampa msaada kwa ushindi kutoka kwake Mola Subhanahu Wataala na akagharikisha mali za wale waliowasaidia majabari. Amechaguliwa Imam mwaka 906H na akabakia katika hali hiyo mpaka mwaka 942H kwa hivyo umedumu uimamu wake miaka thalathini na sita kisha akachaguliwa mtoto wake baadaye:


30) Imam Barakat bin Mohammed bin Ismaeel:

Amechaguliwa baada ya kufa kwa baba yake na akafata njia yake hata alipokufa mwaka 964H baada ya kutawala miaka ishirini na mbili. Na ulikuwa uimamu wa maimamu wawili hawa kitenganisho baina ya vipindi viwili vya utawala wa dhulma na ukandamizaji ambao baada ya kuweko utawala mbaya hapo mwanzo ulikuja tena baada ya hawa maimamu wawili waadilifu. Hawa watawala waliohukumu kwa dhulma ni Bani Nabhan. Katika kipindi hichi cha utawala mbaya walitokea maimamu waliotawala lakini hawakudumu sana kwani hawakuweza kuvumilia dhulma iliyoenea wakti huo. Basi Bani Nabhani walitawala na utawala wao ulikuwa wa ukandamizaji, vitisho na kufanya maafa makubwa kwa viumbe vya Allah Subhanahu Wataala na mwishowe wakapigana wenyewe kwa wenyewe na wakati wao umefunikwa na vumbi la dhulma mpaka Allah Subhanahu Wataala akajaalia kumleta Oman:


31) Imam kiongozi Nasser bin Murshid Al-Yarubiy:

Akarudisha tena sira ya watu wema waliopita katika Oman. Akaleta upya mwendo mzuri wa kinabii ukiwa umevikwa taji ya Imani, mwendo ambao ulitoweka kabisa kwa sababu ya udhalimu uliokuwa hapo nyuma. Ikawa Oman kwa kuja kwa Imam huyu kama kwamba imezaliwa upya na, Allah Subhanahu Wataala akamsaidia kwa kumuwekea watu  wazuri mfano wake(huyo Imam) katika kutenda mema, uchaji Mungu, wivu katika dini na maarifa. Naye alifanikiwa kufanya mengi mazuri, ambayo hawakufanya wenzake kwani aliwatoa Wareno (wa-Portugizi) Oman na akaisafisha kutokana nao. Na watu waovu na maasi wa Oman wenyewe wakajaribu kumpiga vita lakini aliwashinda basi yakanyooka mambo na akafariki - Allah Subhanahu Wataala amrehemu - katika hali  Waisilamu wako radhi nae na umri wake zaidi ya miaka arubaini. Ametawala kutoka mwaka 1024-1050H. kwa hiyo umedumu uimamu wake miaka 26 kisha akachaguliwa mtoto wa Ammi yake:


32) Sultan bin Saif wa kwanza:

Amechaguliwa katika siku ile ile aliokufa Imam Nasser naye alikuwa askari kiongozi wa Imam Nasser na alikuwa chini yake na katika wakati wake aliwafukuza Wareno na akafungua mji wa Sur na vile vile nchi nyingi zilizokuwa zimemilikiwa na India. Kadhalika aliwafukuza hawo Wareno kutoka Mombasa, Kilwa, Zanzibar, Yemen na nchi nynginezo zilizokuwa zimefunguliwa. Akaishi na hali raia wako radhi nae mpaka kufariki kwake siku ya kumi na sita ya Dhil-Qeeda  1091H. ulidumu uimamu wake miaka arubaini na moja. Basi ni ya Allah Subhanahu Wataala miaka hii nini ukubwa wa baraka zake na nini wingi wa harakati zake katika mashariki ya dunia na magharibi yake na kusini kwake …… na kama hivyo. Naye ndiye aliyejenga ngome ya Nizwa iliyonyanyuliwa juu, na yenye msingi wenye nguvu na iliokuwa tabu kupatikana na maadui. Kisha akachaguliwa Imam:


33) Balarab bin Sultan bin Seif

Alikuwa amepambwa na tabia nzuri na fadhila za kupendeza na vitendo vizuri (vyema). Aliona kuwa Oman imejaa mambo mengi mazuri isipokuwa ilipungua katika upande wa kufundisha sharia basi akajenga ngome ya Jibriin ilio na mandhari ya ajabu, iwe madrasa watoke wanavyouni humo ambao watajaza hizo sehemu zilizokuwa tupu zinahitajia watu wasomi. Ameijenga kwa mamilioni ya pesa kitu kinachoonesha utajiri mkubwa uliokuwapo wakati huo. Kadhalika alihifadhi humo ndani pesa zilizofika kiwango kama hicho ambazo zilikuwa zitumiwe wakati wa haja. Uhodari uliotumika katika ujengaji wa ngome hii ni wa kustajaabisha na ingalipo mpaka leo. Limerudishiwa kutengezwa katika wakati huu kwa amri ya Sultan Qaboos. Amechaguliwa Balarab kuwa Imam mwaka 1091H na akatawala hadi mwaka 1104H kwa hivyo alidumu katika uimamu miaka 13.


34) Imam Seif bin Sultan bin Seif.

Ameitwa kwa jina la “pingu ya ardhi” amesema Sheikh Salim bin Humood: “Usifikirie kuwa hili jina la pingu ya ardhi amepewa bure bila ya sababu nalo ni jina kubwa alilopewa kwani ametikisa upeo wa mashariki mpaka sehemu za mbali za Afrika n.k.”. Ameunda majeshi kwa kujiweka tayari kwa vita, hata ikiwa katika mgutio wa mwanzo wa vita farasi elfu tisini na sita 96,000 wako kando yake tayari. Akaingia na jeshi hili India na kuichukua pwani yake kisha akaingia katika ‘Rasi ya Matarajio Mema’ (Cape of Good Hope) hapa ni pale inapokutana bahari kubwa ya Atlantic na bahari ya India. Ametengeza mifereji mingi Oman. Naye amechaguliwa siku ile ile aliekufa ndugu yake mwaka 1104H na akatawala muda wa miaka 19 na kifo chake kilikuwa tarehe 3 Ramadhani mwaka 1123H siku ya Ijumaa. Nasema: “Maimamu hawa wanne wamekamilisha miaka mia wakaijaza nuru Oman na kuitengeza kwa uadilifu (usawa) na kwa majengo wakaifanya kuwa pepo ya dunia Allah Subhanahu Wataala awalipe kila la kheri na Pepo zilizokuwa upana wake ni Mbingu na ardhi”.


35) Imam Sultan bin Seif bin Sultan. Ajulikana kwa Sultan bin Seif wa pili.

Amekuja Oman na hamu yake aigeuze iwe kama mabustani mawili ya “maarib” naye ndiye mwenye kauli mashuhuri: “Akiniweka Allah Subhanahu Wataala hakika nitamfanya msafiri wa Al-Hajji atoke bila ya kuchukuwa zaad (chakula na mahitajio mengine).” Nikasema: wakati huo alioutamani ni huu wakati wetu wa karne ya kumi na tano. Amechaguliwa kuwa Imam siku aliokufa baba yake mwezi wa Ramadhani mwaka 1123H na akafariki siku ya Jumatano tarehe tano Jumadi Al-Akhera mwaka 1131H na umedumu uimamu wake miaka saba na miezi tisa na kwa kufa kwake ikaingia shari Oman na wakahuisha ujahiliya na wakataka kuufanya utawala wa nchi mirathi ya kurithiana.


36) Imam Mohanna bin Sultan bin Majid Al-Yaarubiy:

Naye ni katika watoto wa Ammi wa maimamu waliopita na amemwoa bint wa Imam Seif bin Sultan, na wamemuona waislamu afaa kuwa Imam wakamchagua katika siku aliokufa alie kabla yake Imam Sultan mwaka 1133H baada ya kutawala miaka miwili.


37) Imam Yaareb bin Balarab bin Sultan bin Seif:

Katika watoto wa maimamu waliopita amechaguliwa mwaka 1134H na katika wakti huu wakagawika wa Omani vikundi viwili: Malghafiriy na Mahinawiy. Walipigana Mohammed bin Nasser Al-Ghafriy na Khalaf bin Mubarak Al-Hinaaiy. Waliomfuata Al-Ghafriy katika makabila wakawa Maghafriy na waliomfuata Al-Hinay wakawa Mahinawiy mgawanyiko wa kishetani uliokuwa na mafanikio makubwa sana bila ya mfano. Wakapigana kwa ajili ya hayo wakafa maelfu ya wa Omani. Basi kwa msiba huu mkubwa hakuna isipokuwa tuseme Inna lillah wa Inna Ilaihi raajiuun.




38) Imam Mohammed bin Nasser bin Aamer Al-Ghaafri:

Huyu ndiye aliyepigana vita na Khalaf bin Mubarak kwani wanavyuoni wa Oman waliona katika mtu huyu nguvu na ushujaa wakamchagua kuwa Imam wa Difaa (Himaya). Amesema Imam Nuru Ad-Diin Assalmiy: “Waislamu waweza wakamchaguwa Imam wa Difaa mtu asiyekuwa na walaya (Asiyependwa kwa ajili ya Allah Subhanahu Wataala kwa sababu mwendo wake haukustaqim) ili apate kuwarudi watu wabaya (wanaotaka kuleta fitna kwa nchi) wanaweza wakaendelea naye baada ya fitna hii kutoweka ikiwa mwendo wake utastaqim au sivyo wamuondoe na wamchague Imam mwingine. Amechaguliwa Imam huyu tarehe 7 Muharram mwaka 1137H lakini hakustarehe kwa vita hata siku moja katika kipindi chake cha utawala. Siku moja wakakutana yeye na mpinzani wake Khalaf mbele ya mlango wa ngome ya Sohar wakauliwa wote wawili wakati mmoja. Basi ikapumzika Oman nao lakini haikupumzika na mwito wao mbaya kwani kila damu inayomwagika kwa ajili ya mwito huu hata baada ya kufa kwao wabeba wao sehemu ya madhanbi haya.


39) Imam Seif bin Sultan bin Seif:

Mtoto wa Imam wa thalathini na tano na alikuwa mdogo wakati alipokufa baba yake, hapo ndipo alipochukulia sababu Mohammed bin Nasser kupigana kwa kuwa huyu ni Imam hata angali mdogo lazima atawale na asili ya kupigana kwake sababu yake ni hii. Kisha akachaguliwa yeye mwenyewe badala ya huyo aliyempigania. Lakini hakuachana nae muda wote aliokuwa akipigana. Baada ya kuuliwa Mohammed bin Nasser alikuwa Seif bin Sultan keshabaleghe basi wakamchagua wanavyuoni wa zama zake kwa kuepusha mbali michafuko na akastaqim mwanzo baadae akabadilika basi wakamtoa katika uimamu mwaka 1145H na wakamweka mtoto wa ammi yake:


40) Imam Balarab bin Hamyar bin Sultan bin Seif:

Kitu kilichomkasirisha Seif ndipo alipoifata ile fikra ya watu inayosema: “Bora kukufuru kuliko kukubali kushindwa” basi akasafiri kwenda Makraan akaja na Mabulushi wamsaidie. Lakini walishindwa na akenda Iran akaja na Waajemu, wakateremsha jeshi lao Khorfakan katika mwezi wa Dhul-Hijja mwaka 1149H akaja Imam Balarab kuwahujumu mwezi wa Muharram mwaka 1150H vikatokea vita baina yao na kumalizika kwa kushindwa Imam na wenzake na wakapata watu wa Oman mtihani mkubwa kwa hawa Maajemi jinsi walivyoeneza ufisadi hata huyo aliyowaleta, yaani Seif hakuweza kuwamiliki basi ikabakia Oman katika idhlali kubwa chini ya hawa Maajemi mpaka ukapepea upepo wa Imani wakakusanyika wanavyuoni kutoka kila mahala katika mji wa Nakhal wakawafikiana juu ya Imam:


41)        Sultan bin Murshid Al-Yaarubiy:

Amechaguliwa mwaka 1154H usiku wa kuamkia Arafa. Akasimamisha haki na kuwa katika nguvu kwa idhini ya Allah Subhanahu Wataala zikaanguka ngome chini ya utawala wake, akasimama dhidi yake Seif bin Sultan kama alivyosimama dhidi ya aliye kabla yake. Lakini alishindwa katika mapambano yote na huo ndio ukawa mwisho wake na akafa na hali yuko chini ya zimamu ya Maajemi ambao wamefanya Oman vitendo viovu vilivyokuwa havikufanywa kabla yao. Haya ni matokeo ya vitendo vya watu wajinga ambao hawajali misiba gani watasababisha kwa watani wao na nafsi zao. Akafa yeye na Imam Sultan bin Murshid katika wakati mmoja na Waajemu wanaendelea na ufisadi wao mpaka Allah Subhanahu Wataala akajaalia kuja kwa shujaa katika Mashujaa wa Oman mwenye nguvu, ushujaa na mwenye kuwa macho:


42)        Imam Ahmed bin Saeed Al-Busaidiy:

Babu wa ukoo wa kifalme unaotawala sasa Oman. Akawan’goa Waajemu na kuwafukuza Oman na kuwafanyia ihsani watu wa Oman. Kwa hivyo amepata Ahmed bin Saeed kwa wa Oman mahala pa juu na ikawa daraja yake kubwa mbele yao na kuwa na sauti kwao mpaka akavikika taji ya haiba ya wafalme. Hapo akamtokea yule Imam wa arbaini Balarab bin Hamyar baada ya kuwa alijificha siku za nyuma kwa kuwahofu Waajemu, eti sasa hivi ndio ataka kupigana na Ahmed yakatokea mapigano baina yao yakamalizika kwa kufa kwa Balarab mwaka 1167H. Wakaishi watu katika siku zake katika raha na starehe baada ya kupata kila aina ya mitihani na balaa. Alichaguliwa kuwa Imam baada ya mchuano mkubwa na waajemu na watu wa Oman, na huko kuchaguliwa kwake kulikuwa baada ya kuuliwa Balarab na akadumu katika uimamu miaka ishirini na tisa mpaka kufa kwake mwaka 1196H. Baada ya hapo waliendelea watoto wake kuhukumu mpaka alipochaguliwa:


43)        Imam Azzan bin Qais bin Ahmad:

Mjukuu wa Imam aliye kabla yake, naye kachaguliwa katika mwaka 1285H siku ya Ijumaa, Ishirini na mbili mwezi wa Jamaada Al-akhera. Amesema Imam Noor Ad-Diin: “Hakika uimamu wake ulikubaliwa kwa ujumla (sauti kubwa)”. Akafanya yale yaliyomwajibikia katika kuinusuru dini, kusimamisha haki, na kuwatia adabu madhalimu. Akaingia katika mapigano mengi dhidi ya wa Omani na washambulizi wa Najd, akachukua mali za madhalimu na kuzitia katika “Beit almaal” ya waislamu. Kafanya hivyo baada ya kukubaliana na wanavyuoni wa zama zake. Akabakia Imam mpaka alipokufa shaheed katika usiku wa nane wa Dhil-Qeeda mwaka 1287H baada ya kuhukumu miaka miwili na miezi minne na siku kumi na tano Allah Subhanahu Wataala ampe radhi zake, amin. Alibakia baada kufa kwake muda wa siku tatu hajazikwa na juu ya hivyo hakubadilika.


44)        Imam Salim bin Rashid bin Suleiman bin Aamer Al-Kharusiy:

Amechaguliwa tarehe kumi na mbili katika Jumaada Al-Akhera mwaka 1331H. Alikuwa madhubuti katika hukumu zake na alikuwa haogopi kwa ajili ya Allah Subhanahu Wataala lawama za yoyote yule. Ameiwacha dunia (Zaahid) inaonekana nuru katika kiwiliwili chake yungali yuhai. Akasimama pamoja na haki kuamrisha mema na kukataza mabaya na kuwatia adabu wenye makosa na ikaendelea Oman katika wakti wake na ikazidi baraka. Kabakia katika Uimamu mpaka alipokufa shaheed katika usiku wa tano wa Dhil-Qeeda mwaka 1338H. Ulikuwa uimamu wake miaka saba na miezi minne na siku ishirini na mbili.


45)        Imam Mohammed bin Abdallah bin Saeed Al-Khaliliy:

Amechaguliwa baada ya kufa aliekuwa kabla yake kwa siku saba katika Dhil-Qeeda 1338H. Alikuwa ana elimu zaidi kuliko watu wote katika wakati wake, akatimiza masharti yote yanayotakiwa kwa msimamiaji wa haki (Mtawala kwa sharia ya Kiislamu) akafanya waajibu wake kadri ya uwezo wake, akapigana na wezi wa marabarani (wanaowakatia watu njia), akaleta amani nchini na kusimamisha mipaka ya dini kama walivyosimamisha maimamu walio kabla yake, na akaishi hali ya kuwa marejeo kwa watu wa Oman. Ametoa mali yake yote katika kuitia nguvu nchi na alikuwa tajiri kwa kuachiwa urithi na baba yake na akafa hamiliki kitu. Amekufa usubuhi wa siku ya Ishirini na tisa Shaaban mwaka 1373H na Uimamu wake ulidumu miaka thelathini na nne, miezi tisa na siku kumi na saba na alimchagua kuongoza umma Imamu (kabla ya kufa kwake) kwa sababu ya fujo na mizozo ilioko wakti huo.


46)        Imam Ghalib bin Ali bin Hilal Al-Hinaaiy:

Ni pekee katika maimamu alichaguliwa na Imam alie kabla yake (Imam Mohammed bin Abdallah bin Saeed Al-Khaliliy). Akaingizwa katika uimamu kabla ya kuzikwa aliemtangulia. Alifanya wajibu wake kwa umma isipokuwa kadari (hali ya mambo yaliotokea) haikumsaidia. Maafa yaliyompata ni sawa sawa na yale yaliyompata Imam Assalt bin Malik. Naye hakutawala isipokuwa miezi kumi na nane.


Maimamu hawa ndio waliokubaliwa na  wote (ijmaa). Amma wana tarehe wa Kiomani wamehesabu maimamu sitini lakini hatukutaja hapa isipokuwa wale mashuhuri.




Imeenea madhehebu ya Kiibadhi katika nchi za magharibi za Kiarabu (Libya, Tunisia na Algeria).

Tutataja hapa kwa kutoa mfano tu sio kwa ajili ya kuzingatia majina ya wote hao waliochukua elimu kupeleka nchi za magharibi:

Waliochukua elimu na dini kutokana na Imam Abi Ubaidah Muslim bin Abi Kariimah ni:-

Abu Ubaidah Abd Al-Hameed bin Mughteer Al-Janaawiniy, Imam Abu Al-Khattab Abd Al-Aaala bin Assamh Al-Maafiriy naye ni Imam wa kwanza wa nchi hizi za magharibi. Amechaguliwa kuwa Imam mwaka 140H na Imam Abd Arrahman bin Rustum Al-Faarsiy (Tai wa Uajemu) amechaguliwa imamu mwaka 160H katika Taihert Algeria ambayo yalikuwa ndio makao makuu ya Uimamu huu wa Kirustum katika kaskazini ya Afrika kisha wakachaguliwa watoto na wajukuu zake kuwa maimamu kwa ajili ya elimu, fadhli na uongofu wao. Kadhalika Abu Dawood Al-Qabaliy Annafzaawiy, Ismaaeel bin Draar Al-Ghadaamsiy na Aasim Assaddraatiy na hao wote ni katika wale waliochukua elimu kuipeleka nchi za Magharibi za kiarabu.


Kisha wakafuatia baada ya waliotajwa nyuma wanavyuoni wakubwa tokea wakati huo mpake leo hii. Anachukua elimu ya dini yule aliechelewa kutoka kwa yule alietangulia. Katika hao ni:-

Imam Abdilwahab bin Abdirrahman bin Rustum, Imam Aflah bin Abdilwahab, Imam Mohammed bin Aflah bin Abdilwahab, Abu Mirdas Mahasir Assidratiy, Abu Dhar Abaan bin Wasiim, Amroos bin Fath Almasaakniy, Abu Khalil Addarkaliy, Abu Al-Muniib Mohammed bin Yaanis, Abu Al-Qaasim Albaghtooriy, Abu Khirz Yaghlaa bin Zaltaaf, Abu Nooh Saeed bin Zangheel, Abu Abdallah Mohammed bin Abi Bakr, Tabghuooriin bin Eeisa Almalshootiy, Abu Arrabii Suleiman bin Yakhlef, Abu Ammarr Abd Al-Kaafiy, Abu Yaaqoob Yousuf bin Ebrahim Al-Waarijalaaniy, Abu Nasser Fath bin Nooh Al-Malooshaaiy, Abu Al-Qassim Al-Barraadiy, Ahmed bin Saeed Asshammaakhiy, Ahmed bin Saeed Addirjiiniy, Yahya bin Sufyaan Al-laaloootiy, Abu Haaroon Al-Jalaalimiy, Abu Arrabii Suleiman bin Haaroon, Abu Yahya Zakaria bin Ibrahim Albarooniy, Eesa Attarmiisiy, Abu Saakin Aamer bin Aliy Asshahammakhiy, Abu Taahir Ismaaeel bin Musa Al-Jaytaaliy, Dawood bin Ibrahiim Attalaatiy, Yaaqoob bin Ahmed Al-Yafraniy, Abu Yahya Al-Janaawiniy, Mahdiy bin Esmaeel, Abdullah bin Mohammed Al-Majdaliy, Abdul Aziz Atthamiiniy, Ibrahiim bin Yusuf Atfeysh. Mohammed bin Yusuf Atfeysh (Qutb Al-Aimmah), Abdullah bin Yahya Al-Baarooniy, Abu Al-Yaqdhaan Ibrahiim bin Issa, Ibrahiim bin Omar Bayyoodh, Abdallah Bakliy, Aliy Yahya Muammar na wengineo wengi.


Wamesimamisha Maibadhi katika nchi za Magharibi ya Uarabu uongozi wa uadilifu na Imam wa kwanza alikuwa Abu Al-Khattab Al-Maafiriy kisha Imam Abu Haatim Al-Malzooziy halafu ukaja Uimamu wa Kirustum ulikuwa mashuhuri. Nchi zilizopata hadhi ya kuwa chini ya uongozi huu wa uadilifu ni Waarjalaam katika Algeria, Jarba katika Tunnis na Jabal Nafuusa katika Libya. Wakaunda nidhaamu ya kutawala (Nidham Al-Azzaba) na ni mpango mzuri sana ndio uliohifadhi fardhi ya kuamrishana mema na kukatazana na mabaya katika nchi hizi. Na mpango huu ulikuwa na athari kubwa sana katika kuhifadhi Istiqama katika nchi hizi.




Madhehbu hii kadhalika imeenea huko Yemen na ikapata watu wakubwa waliopigiwa mifano mizuri katika elimu na vitendo. Amesema juu yao Imam Mwanachuoni Mkubwa Waail bin Ayoub Al-Hadhramiy: “Nimewawahi watu katika Hadhramaut kama ingekuwa mmoja katika wao angepewa uongozi wa Ulimwengu mzima basi angelihimili kufanya hivyo (Augeliweza kutawala bila ya tabu yo yote) kwa ukubwa wa akili, elimu, busara na ucha Mungu wake”.


Katika hao Imam Taalib Al-Haqq Abdallah bin Yahya Al-Kindiy Imam wa kwanza katika Yemen. Amechaguliwa mwaka 129H, Abraha bin Assabaah Al-Hameiriy, Abdallah bin Saeed, Waaeel bin Ayoub, Abu Almuarij Amrou bin Mohammed Assodousiy, Qais bin Suleiman na Imam Ibrahiim bin Qais Al-Hadhramiy. Amesema Imam Noor Ad-Diin Assalmiy katika shairi: “Wa Omani, Wa Magharibi na Wa Hadhramaut wana wengi katika viongozi wao, wanaofanana na Omar wawili katika Uadilifu, kumkhofu Allah Subhanahu Wataala, uaminifu na tabia nzuri. Wamepita katika njia ilio sawa basi wakapata sifa nzuri (Kusifiwa na raia zao) pamoja na kupata radhi za mola wao Subhanahu Wataala



Ilikuwa madhehebu ya Ibaadhi imeenea huko Khurasaan wakawa wanao wanavyouni, kadhalika Ghana, Magharibi ya Afrika. Bali kwa hakika Uislamu umeingia Afrika ya Magharibi kwa njia ya Maibadhi na katika Afrika ya Mashariki. Kama ilivyokuwa Maibadhi wa Oman wao ndio waliopeleka Uislamu Mashariki ya Asia, ndipo ulipoingia Uislamu huko Arkhabiil Al-Malayo (Malasia) katika mikono yao.


Tuliyoyataja ni mukhtasari ili apate msomaji kujua kuwa madhehebu hii ndio asili. Sio madhehebu ilio chaguliwa na binadamu kwa mapendekezo ya nafsi zao la bali imechaguliwa na Allah Subhanahu Wataala ……na mafinikio yangu hayawi isipokuwa kwa kutaka Mola Subhanahu Wataala.

No comments:

Post a Comment

Note: only a member of this blog may post a comment.