Tuesday, 19 January 2016

Juzuu 2 Salaa----Kujenga Uongofu katika nyoyo za Vijana-----


JEZUU YA PILI


Kasema Allah katika sura Al-Hashr aya ya 7


                 الحشر: ٧

“Na anayokupeni Mtume basi pokeeni na anayokukatazeni jiepusheni nayo”



Kupunguza Sala zenye rakaa 4 – Adhuhuri, Al-Asiri na AI-Isha.

Ni wajibu kwa msafiri kupunguza Sala hizi wala si ruhusa (khiari) kama hali ilivyo katika funga ya Ramadhani kwani msafiri amepewa ruhusa ya kufungua (ikiwa atapata mashaka katika safari) kwa mujibu wa kauli ya Mtume Salallahu Alayhi Wasalam na kitendo chake. Ama kauli yake amesema:-

 فرضت الصلاة ركعتين ركعتين فأقرت في السفر وزيد في الحضر أربعاً ) (

"Imefaridhishwa Sala rakaa mbili mbili, ikathibitishwa katika safari na ikaongezwa kuwa rakaa nne katika watani. (Ni lazima Muislamu kuchukua watani – mahala anapotulia na kuishi ndani yake yaani anakuwa sio katika hali ya safari.)"


Vile vile amesema Mtume Salallahu Alayhi Wasalam:-

( على المقيم سبع عشر ركعة وعلى المسافر إحدى عشرة ركعة )

"Mkaazi (katika watani wake) ni wajibu asali rakaa kumi na saba na ni wajibu wa msafiri kusali rakaa kumi na moja."


Amma kwa mujibu wa kitendo chake katika kupunguza Sala, ametoa hadithi Ibn Abbas kuwa Mtume Salallahu Alayhi Wasalam alikaa Makka katika mwaka wa Al-Fat-h (mwaka iliyofunguliwa Makka) siku kumi na tano anapunguza Sala naye hana niya ya kukaa ndani yake. Ikaendelea hali hii ya kupunguza Sala katika wakati wa Makhalifa waliokwenda mwendo mzuri (Arrashidiin).


Mtume Salallahu Alayhi Wasalam alitoka siku moja baada ya kusali Adhuhuri huko Madina rakaa nne, na akaelekea Dhul -                           Huleifa akasali huko Al-Asiri rakaa mbili kisha akarejea. (Hii Dhul-Huleifa iko mwendo wa farsakhi mbili kutoka Madina (kilo meter 12 ndio mwendo ambao baada yake inapunguzwa Sala) na akasema Salallahu Alayhi Wasalam: Nimekuja ili niwafundishe Sala ya kupunguza (Inayosaliwa safarini).

Kwa hivyo ni wajibu kupunguza Sala baada ya kusafiri kwa masafa (mwendo) ya farsakhi mbili (sawa na kilometer 12). Na waliotutangulia walikuwa wakichukua hima kubwa kuyapima haya masafa, na walikuwa wakipanda punda au ngamia na huku wakiburuza kamba yenye urefu ujulikanao na huku wakitia alama hivyo hivyo mpaka utakapokamilika mwendo wa kupunguza Sala. Na anayesali katika safari zile Sala za rakaa nne (Adhuhuri, Al-Asiri, Al-Ishaa) akazisali hivyo hivyo rakaa nne (bila ya kuzipunguza) ni sawa na aliyesali rakaa mbili katika watani wake (akiwa kwao) yaani Sala yake haitimii. Baadhi ya waliokuwa hawajui husema:- Ziada ni bora kuliko kupunguza yaani kusali rakaa nne ni bora kuliko rakaa mbili na huu ni ujinga mkubwa unaonesha kutofahamu sharia ya Dini. Wengine wasema nchi za kiarabu zote ni watani, maneno haya si kweli wala hayana msingi wowote katika Dini. Wengine wasema: Hawachoki katika safari na kupunguza Sala imeletwa kwa ajili ya taabu kama ilivyokuwa safari juu ya punda na wanyama wengine, hii inaonesha upungufu wa maarifa. “Na hakiwi kinachozidi kuliko Qur'ani isipokuwa upungufu.”

Na Mtume Salallahu Alayhi Wasalam hakufa ila baada ya kuteremka kauli yake Allah Subhanahu Wataala:


        المائدة: ٣

“Leo nimekukamilishieni Dini yenu”


Na yeye Mtume Salallahu Alayhi Wasalam ndiye aliyetuletea faridha ya Sala kutokana na amri ya Allah Subhanahu Wataala kwa hivyo aliyotuamrisha ndiyo tunayoyafuata na wala haitufalii kuongeza kitu chochote kwa uzushi wetu wenyewe kwani akili zetu hazifikii kiwango hichi. Basi tusimame katika mpaka wetu tulioekewa na sharia yetu ikiwa twataka mafanikio yetu.


Mkaazi katika mji kwa ajili ya kazi na akawa hakutia nia ya kuishi katika mji huo bali ikimalizika kazi yake arejea katika watani wake basi huyu asikamilishe Sala zake (zile za rakaa nne asali rakaa mbili) isipokuwa ni bora asali kila Sala kwa wakati wake yaani asichanganye baina ya Sala mbili. Asali Adhuhuri katika wakati wake rakaa mbili, Al-Asiri rakaa mbili na Al-Ishaa rakaa mbili, isipokuwa akisali nyuma ya Imamu ambaye ni mkaaji wa mji huo basi asali kwa mujibu wa Sala ya Imamu (yaani akamilishe).


Kusali (kwa msafiri) kila Sala kwa wakati wake na kuchanganya (Sala mbili pamoja) yote mawili ni sunna, lakini ni bora kwa anayeishi ugenini kusali kila Sala kwa wakati wake na kwa aliye mbioni safarini kuchanganya. Hivi ndivyo alivyokuwa Mtume Salallahu Alayhi Wasalam akifanya (Adhuhuri na Al-Asiri  akizisali pamoja, na Al-Maghrib na Al-Ishaa akizisali pamoja, na Al- Fajiri husaliwa peke yake). Asiyekuwa na kwao (watani) huwa hana Sala kwa hiyo ni lazima kila mtu awe na watani wake. Na katika masharti ya watani ni kuwa huondoki humo isipokuwa kwa dharura.



Ni wajibu wa kila anaeingia msikitini akakuta Sala ya jamaa yasaliwa kujiunga nayo, siyo kusubiri mpaka ikamalizika au kusali peke yake wakati bado Sala ya jamaa imesimama; hivi haijuzu.


Akishaifikia safu atasoma tawjihi (na huku ametia nia moyoni ya kusali Sala Fulani ile anayotaka kuisali).

 ( سبحانك اللهم وبحمدك تبارك اسمك وتعالى جدك ولا إله غيرك إني وجهت وجهي للذي فطر السموات والأرض حنيفا وما أنا من المشركين )


Kisha atapiga Takbira Al Ihram. Ikiwa Imamu asoma Al Hamdu naye vile vile asome Al Hamdu. Na ikiwa Imamu asoma sura (baada ya Al-Hamdu) yeye asikilize asisome kitu kisha ailipe Al Hamdu (kwa kuisoma baada ya Imamu kutoa Salamu yeye anyanyuke na aisome). Akiwa Imamu yuko katika Rukuu naye arukuu na akimkuta katika Sujuud naye asujudu, akimkuta katika Tahiyaatu ya mwanzo naye akae asome Tahiyaatu, lakini akimkuta katika Tahiyaatu ya mwisho amngojee mpaka atoe Salamu kisha asali peke yake.


Vile vile afanye ikiwa kaingia msikitini akaikuta jamaa na Imamu yuko katika rakaa ya pili kwa mfano, yaani asome Tawjih kisha apige Takbirat Al Ihram asome Audhu na asome Al-fatiha kisha arukuu pamoja na Imamu na amfuate mpaka atakapotoa Salamu. Akitoa Salamu Imamu asimame aliyeunga Sala bila ya kutoa Salamu kisha asome Al-Hamdu ikiwa Sala ya mchana na Al Hamdu na sura ikiwa Sala ya usiku, kisha arukuu halafu asujudu sijda mbili kisha asimame kwa takbira mpaka atulie katika kisimamo chake bila kusoma kitu; hapa ndipo mahala alipojiunga na Imamu. Basi hapo akae na atoe Salamu. Na hivyo hivyo afanye akiingia katika Sala ya jamaa katika rakaa ya tatu au ya nne. Aijalie mwisho wa Sala yake mwisho wa Sala ya Imamu kisha alipe kilichompita yaani tokea mwanzo wa Sala mpaka pale alipojiunga na Imamu.


Vile vile ikiwa amejiunga na Imamu katika rakaa ya kwanza kwa mfano katika rukuu ya kwanza asome Tawajiih kisha apige Takbira ya Al-Ihram na arukuu pamoja na Imamu na amfuate mpaka atoe Salamu lakini yeye asitoe Salamu bali asimame na asome Audhubillahi mina shaitani arrajim kisha asome Al Fatiha katika Sala ya mchana na Al Fatiha na sura katika Sala ya usiku kisha akae (kikao cha Attahiyatu) halafu atoe Salamu. Na akimkuta (akajiunga na) Imam katika mwanzo wa rakaa ya pili au ya tatu au ya nne basi baada ya kutoa Salamu Imamu lazima asimame (bila ya kutoa Salamu) ainuke ule muinuko uliompita kisha akae kama tulivyoeleza kwani kuulipa ule mwinuko ndio kukamilisha Sala, bila yake haitimii, lazima azingatie kitu hichi.


Na akikuta safu imejaa (mstari wa watu wanaosali nyuma ya Imamu) hapana wasaa wa yeye kuingia ndani yake basi na asimame nyuma ya safu asome Tawjiih na kabla ya kupiga Takbira ya Al-Ihram amvute mmoja katika wanaosali safu ya mbele na akishakuwa amesimama kando yake basi apige Takbira ya Al-Ihram na asipige kabla hajasimama kando yake kwa sababu baada ya Takbira haimjuzii kufanya kitendo chochote na asicheleweshe kupiga Takbira baada ya kufika sahibu yake kando yake kwani itamharibia Sala yake. Azingatie mambo haya.



Sala ya Jamaa ni faradhi kwa kila Muislamu kutokana na Aya za Qurani na Hadithi za Mtume Salallahu Alayhi Wasalam na juu ya hayo ni nuru kwa Muislamu. Sala moja ya jamaa ni sawa sawa na Sala ishirini na saba ya kusali mtu peke yake.

Walikuwa baadhi ya watu wema wakilia zikiwapita Sala za jamaa, na baadhi yao wazigharimu nafsi zao kwa kuisali Sala hiyo hiyo mara ishirini na saba wakipitwa na Sala ya jamaa, yaani katika hizi Sala moja ni faridha na zilizobakia ishirini na sita ni “naafila”, na juu ya hivyo kajiona katika ndoto yuko nyuma na wenzake (waliosali jamaa) wamemtangulia. Vile vile mwenye kuacha Sala ya jamaa bila udhuru hukataliwa na Waislamu wala haikubaliwi shahada yake wala hapewi “walaa” (kupendwa na Waislamu, kuhurumiwa na kuombewa Dua ya maghufira na ya kuingizwa Peponi, akiwa hayi na akifa)


Kwa hivyo anaepoteza Sala ya Jamaa kwa kazi yake au mchezo wake kama kushughulishwa na biashara yake, kuendesha gari yake, kutizama mpira (football), upuuzi wa T.V au mengineyo kama kujiona nafsi yake bora hawezi kuchanganyika na watu wengine, hao wako katika hasara kubwa na ya uwazi watakuja Siku ya Kiyama wana majuto makubwa siku iliyokuwa hayafai majuto.

Na tunatoa mfano wa hayo:-

Kikundi cha watu kimesafiri na kila mmoja katika wao kachukua katika safari yake hiyo chakula na anachokihitajia ndani yake isipokuwa mmoja wao hakuchukua kitu. Je mtu huyu hataona haya wakati wakimsaidia kumpa chakula chao? Na ikiwa hawakumsaidia atashikwa na njaa.



Sala za sunna ambazo hazina budi kusaliwa kuna zilizotiliwa nguvu (سنن مؤكدة) na kuna zisizotiliwa nguvu (سنن غير مؤكدة).

Zilizotiliwa nguvu:

Zilizotiliwa nguvu ni zile ambazo Mtume Salallahu Alayhi Wasalam alizisali bila ya kuziacha popote alipokuwa - safarini au kwake. Hizi ni sunna ya Al-Fajiri rakaa mbili kabla ya faradhi, Salaa ya witri ambayo husaliwa baina ya Sala ya Al-Ishaa na ya  Al-Fajiri, na sunna ya Magharibi kwa aliyeko kwake ( siyo kwa aliyeko safarini ) rakaa mbili baada ya faridha .



Sala za Idd husaliwa rakaa mbili; hupigwa takbira tano baada ya Takbira Al-Ihram kisha husomwa Al Hamdu na sura, katika rakaa ya pili husomwa Al Hamdu na sura halafu hupigwa Takbira tano kisha kurukuu na baada ya kuinuka kwenye rukuu kabla ya kusujudu hupigwa takbira tatu na kwa hizo hutimia takbira kumi na tatu (za ziada). Kisha Imamu atatoa hotuba ifaayo.



Husaliwa maiti kwa Takbira nne bila kurukuu wala kusujudu. Kwanza hupigwa Takbira Al-Ihram baada ya Tawjiih kisha inasomwa Al-Hamdu halafu Takbira ya pili kisha yasomwa Al-Hamdu halafu hupigwa Takbira ya tatu na baada yake husomwa Dua ya ujumla kwa huyo maiti kama kauli yake Mola Subhanahu Wataala:


                                                                ﭜﭝ                 ﭤﭥ                 ﭫﭬ                غافر: ٧ - ٩

Ataongeza kwa muombea maiti aliekuwa katika “Walaa” (Anaependwa na kuridhiwa na Waislamu kwa msimamo wake mzuri katika Dini mpaka kufa kwake) kwa kumuombea Pepo na radhi ya Allah Subhanahu Wataala kisha ajiombee nafsi yake na Wazee wake wawili kisha hupigwa Takbira ya nne halafu husaliwa Mtume Salallahu Alayhi Wasalam kisha hutolewa Salamu hafifu (kwa sauti ndogo).


1- Sala ya Tahiyatu Al Masjid rakaa mbili, nayo husaliwa akiingia mtu msikitini na asome ndani yake (baada ya Takbira Al-Ihram) Al-Fatiha na sura katika rakaa zote mbili. Akiingia msikitini na Sala ya Jamaa yasaliwa basi na ajiunge na hiyo Sala ya faradhi na hiyo Tahiyatu Al Masjid haimpasi na vile vile haimpasi ikiwa atasali faradhi peke yake.

2- Sala ya sunna ya Adhuhuri rakaa 2 au 4 kabla ya Sala ya faradhi na rakaa 2 au 4 baada ya faradhi.

3- Sunna ya Al-Asiri rakaa 4 nne kabla ya faradhi.[1]

Haisihi Sala (haifai) yoyote baada ya faradhi ya Al-Asiri mpaka ingie Sala ya Magharibi isipokuwa ikiwa mtu amepitiwa na usingizi bila ya kusali faradhi au kaisahau basi wakati akigutuka au akikumbuka wakati huo huo aisali kwa hivyo hali kama hii haikatazwi kusali baada Al-Asiri kwa hadithi:-

 ( من نام عن صلاة أو نسيها فليصلها متى ذكرها فذلك وقتها )

“Aliyelala wakati wa Sala au aliyesahau basi naasali akumbukapo tu, na huo utakuwa ndiyo wakati wake hiyo Sala.”


Vile vile katika Sala ambazo zawezekana kusaliwa baada ya Al-Asiri (haziingii katika katazo la kusali baada Al-Asiri) ni Sala ya maiti, Sala ya kupatwa kwa jua au mwezi na Sala ya tawaaf; hizi haiwezekani kucheleweshwa.

4- Sunna ya Ishaa nayo ni rakaa mbili baada faridha.

5- Sunna ya Dhuha nayo ni rakaa mbili, nne au nane.

6- Sala ya kupatwa kwa Jua au Mwezi. Husaliwa rakaa mbili na rakaa ya pili huwa fupi zaidi kuliko ya mwanzo, sijda ya pili huwa fupi zaidi kuliko ya mwanzo, nayo huingizwa rakaa nyengine katika kila rakaa na rakaa mbili zikawa nne. Wakati anaposimama kutoka kurukuu katika rakaa ya mwanzo husoma tena kwa ufupi zaidi kuliko mara ya mwanzo kisha arukuu mara ya pili halafu asujudu. Hufanya hivyo hivyo katika rakaa ya pili.


Haya ndiyo tuliyofundishwa na sunna kuyafanya wakati linapopatwa jua na unapopatwa mwezi, sio kama wafanyavyo watu wengi kuadhini njiani, kuwapiga wanyama na watoto mpaka walie, kupiga ngoma na kupiga makelele kwa sauti kubwa wanafikiria wakifanya hivyo wanawapasha habari Malaika kuwa mji wao umejaa watu nao ni Waislamu kwa hiyo wasizamishwe katika ardhi. Imani kama hii ni uzushi ulioletwa na maadui wa Kiislamu. Twamuomba Allah Subhanahu Wataala salama!

7- Sala ya haja nayo ni rakaa mbili.

8- Sala ya Istikhara rakaa mbili.

9- Sala ya Tarawehe katika mwezi wa Ramadhani.

10- Kusali Qiyaam katika theluthi ya mwisho ya usiku ijapokuwa rakaa mbili na kusoma Al-Fatiha na Aya ya Al-Kursiy katika rakaa ya kwanza na Al-Fatiha na Qul-Huwa-Allah-Ahad mara tatu katika rakaa ya pili.


Hizi ndizo Sala za muhimu ambazo zimetokana na Mtume Salallahu Alayhi Wasalam, na uongofu wote wapatikana katika kufuata mwendo wake Mtume Salallahu Alayhi Wasalam na wala hapana kheri kwa asiyefuata mwendo huo na hali aweza.



Sijda ya sahau ni katika mambo yaliyo wajibu kuyafanya ili kuziba makosa yaliyofanywa katika Sala. Na jambo ambalo wajibu hautimii isipokuwa kwa kulifanya basi nalo ni wajibu.

Mfano mtu kasahau katika Sala yake akasimama badala ya kukaa au kinyume chake, au kitu kinachofanana na hicho kisha akakumbuka na akarejea, au ametoa Salamu katika rakaa ya pili badala ya tatu bila ya kuondoka katika mahala pake hapo, wala hakuzungumza bali alipokumbuka akasimama na kukamilisha Sala yake, au vile vile anaesali nyuma ya Imamu naye akasahau katika Sala  yake yote (akili yake haikuwa hadhiri tokea mwanzo wa Sala mpaka mwisho) na hakujua Imamu kasali rakaa ngapi basi husujudu kwa kusahau kama ilivyokuja katika hadithi ya Mtume Salallahu Alayhi Wasalam. Ama akiwa asali peke yake na akasahau asijue rakaa ngapi kasali mpaka kamaliza Sala yake huyu lazima airudie. Na kama ametia shaka wakati yuko katika rakaa ya tatu je yuko katika rakaa ya pili au ya tatu basi na aijalie rakaa ya pili na akamilishe Sala yake, na kama hivyo akitia shaka katika rakaa ya nne je yupo katika rakaa ya tatu au ya nne basi aijalie ya tatu kisha aikamilishe Sala yake halafu asujudu sijda ya sahau.


Sijda ya sahau humghadhibisha sheitani, asema “Ole wangu nimeamrishwa kusujudu na nimeasi na binaadamu kaamrishwa kusujudu na akatii.”

Sijda baada ya Sala inajuzu bila ya kusahau ikiwa haikufanywa kuwa ni katika Sala.

Alikuwa Arrabii Allah Subhanahu Wataala amrehemu asujudu sijida mbili bila ya kusahau lakini husujudu kwa ajili ya mghafala au upungufu ambao unamtokea katika Sala akaupa hukumu ya kusahau.

Asema Ibn Abbas: (Ikiwa aweza mmoja wenu asisali isipokuwa asujudu baada yake sijida mbili basi na afanye hivyo). Lakini kwa sharti asichukulie kuwa ni wajibu. Ndio maana wanavyuoni wetu wa mwisho wameziacha kwa kuogopea watu wasiojua kuchukulia kuwa ni faradhi.




Kugeuka geuka katika Sala

Wengi miongoni mwa wasiojua hugeuka geuka katika Sala na kitu hichi kinaharibu Sala moja kwa moja, wala hakuna asemaye kuwa yajuzu kugeuka katika Sala, na madhehebu ya Ibadhi haijuzishi kitendo chochote katika Sala hata kikiwa kidogo vipi. Sala inabatilika kwa kucheza cheza walau kidogo ikiwa sio kwa ajili ya kuitengeneza hiyo Sala.


Miongoni mwa watu (wema) wako wanapoingia katika Sala wanakuwa hawasikii kitu hata wakipitiwa na wapigaji ngoma, wachezaji  na waimbaji. Na wapo katika Maibadhi miongoni mwa hawa wengi wengi - Allah Subhanahu Wataala awaridhie na awajaalie wawe radhi nae.

Na wala hazingatiwi mtu mjinga na vitendo vyake, kwani Dini haichukuliwi kutokana na wajinga, wala haiwezekani kuwahukumu watu wote kwa mambo yanayofanywa na watu wachache, wala haifai kuwazulia watu wema kitu kisichokuwa cha kweli. (Wako wanaosema kuwa Maibadhi wanachezacheza katika sala na hali imejengwa hukumu hiyo kwa kuwaona badhi ya watu wajinga wanaposali wakahukumiwa Maibadhi wote pamoja na Wanavyuoni wao kuwa ndivyo wanavyosali. Huu ni uzushi mkubwa). Kuna msemo: "Mwenye matusi zaidi katika watu ni yule anayewatukana walio kama yeye". Na Allah Subhanahu Wataala ni Mjuzi wa kila alisemalo mtu, basi na aseme atakalo.


Katika mambo yanayoharibu Sala vile vile:-

Kunyanyua kichwa juu (kutizama juu); wengi katika wasiojua wafanya harakati hii wanaponyanyuka baada ya kurukuu. Vile vile kuteremsha kidevu na kukibanisha na kifua mpaka akawa anaangalia tumbo.

Msimamo sahihi katika Sala ni ifuatavyo:-

Aangalie mtu pale anaposujudu wala asipakiuke kuangalia mbali au karibu zaidi.

Asifumbe macho wala asiyafumbue sana kiasi ya kuwa atashughulika na waliokuwa karibu yake, bali ayajalie baina ya kufungua na kufunga. Na katika kukaa (kikao cha Tahiyatu) asikalie visigino kwani mkao huu wakatazwa na sharia. Na wala asidonoe katika sijida (kusujudu upesi upesi kama jogoo anapodonoa chakula ardhini), na asiseme سبحان ربي الأعلى   chini ya mara tatu katika sijida. Na baina ya sijida mbili akae kwa kituo mpaka kila kiungo kitulie mahala pake na wala asiseme chochote baina ya sijida mbili kwani kauli yoyote hapa huharibu Sala. Na Allah Subhanahu Wataala ndie mwenye kutoa taufiki.


Kuosha Maiti

Katika sunna zilizotiliwa nguvu ni kuosha maiti.



Kumuweka maiti kwenye ubao na astiriwe utupu wake na muoshaji avae kitambaa mkononi mwake.

Ataanza kumsafisha utupu wake kuanzia kitovu mpaka magotini na atie mkono wake chini ya nguo iliyomstiri maiti na amuoshe utupu wake kisha amkalishe maiti na kukama tumbo lake mara tatu na amuoshe ikiwa atatoka uchafu (najisi) wowote. Akisha hakikisha kuwa hana tena najisi amuoshe kwa maji na majani ya mkunazi. Na mwenye kuosha siku hizi kwa sabuni badala ya majani ya mkunazi hakosolewi kwani sabuni yasafisha zaidi kuliko majani ya mkunazi, lakini kuosha kwa majani ya mkunazi ni sunna.

Kisha  amtie udhu wa Sala halafu amuogeshe kwa maji safi kama kuoga janaba, kisha amuogeshe kwa maji yenye manukato kama kafuri au mfano huo. Kwa hiyo itakuwa jumla amemuogesha mara tatu. Na hiyo ndiyo sunna. Kisha amfute maji na amtie katika sanda.



Zichukuliwe nguo tatu nyeupe zilizo tahiri kwa mwanamme: kikoi, kanzu na kilemba. Na kwa mwanamke nguo tano: suruwali, kanzu, ushungi na shuka mbili. Kwanza zitandikwe nguo chini kisha ndio maiti awekwa juu yake na kabla hajafungwa na hizo nguo azibwe kwa pamba katika kila uwazi wa mwili. Inapendelewa kutia manukato katika pamba kisha atiwe machoni, puani, masikioni, mdomoni, na huzibwa uso wake wote kwa pande la pamba. Pia awekewe kwenye shingo, kwapa, kifua, kitovu, kwenye utupu, chini ya magoti na baina ya vidole vya mikono na baina ya vidole vya miguu. Kisha azingirishwe sanda na ifungwe bila ya kukazwa sana.


Inapendelewa akitiwa kaburini alegezwe fundo kwenye macho yake ili awaone Malaika wawili. Na ni katika sunna kulifukiza jeneza kwa udi kwa kulizungushia  kietezo mara tatu kisha ndio achukuliwe na kupelekwa kaburini na awekwe mahala penye tohara na asaliwe halafu azikwe na aachwe baina yake na Mola wake Mkarimu Mrehemevu.


                               الزلزلة: ٧ - ٨

[Basi anayefanya wema hata wa kiasi cha uzito wa mdudu chungu ataona jaza yake. Na anayefanya uovu hata wa kiasi cha uzito wa mdudu chungu ataona jaza yake]



Sala ya Kuomba Mvua (  صلاة الاستسقاء   )

Ni sunna kusali Sala ya kuomba mvua kutakapoingia ukame na kukatika mvua. Husaliwa rakaa mbili na husomwa katika kila rakaa Al-Hamdu na sura nyingine. Kisha husimama Imamu na hutoa hotuba na kumuomba Mola Subhanahu Wataala kwa unyenyekevu na kuogopa ili awaondolee balaa na awaletee mvua ili kuwarehemu waja wake, wanyama na watoto. Na aipindue shuka yake aliyojifunika kama ilivyokuja katika sunna. Na kuipindua shuka ni kuashiria matumainio mema ya kubadilika wakati (kuja wakati mzuri).



Kuondosha vilivyozidi katika mwili kama kukata kucha, kunyonyoa nywele za kwapa na kunyoa nywele za kinena na kupunguza masharubu kwa chini na pembeni mwake. Hayo yote ni katika sunna alizoamrishwa Muislamu kuzifanya, nayo katika usafi yana sehemu isiyofichikana. Kwani vitu hivyo vikiachiwa vizidi vitasababisha uchafu kujikusanya ndani yake. Makucha hukaa vibaya yakitokeza na kuwa marefu, na masharubu yakiwa marefu yanambadilisha mtu sura yake na kuchusha kama anavyochusha mwenye kunyoa ndevu zake au mwenye kuzipunguza au kuzichezea.


Tizama sharia ya Allah Subhanahu Wataala nini manufaa yake na ubora wake. Hakutuamrisha kitu isipokuwa chapendeza na hakutukataza kitu isipokuwa chachusha na kumfanya yule anachokitenda atishe kwa watu na ajihisi mwenyewe yuko chini ya watu wengine, akikaa mbele ya watu wa heshima ajiona dhalili.


Angalia kwa mfano mtu aoaye mke kwa halali huitangazia harusi yake na huwalisha watu chakula na kulala mahala pazuri na godoro zuri katika raha na starehe. Lakini amchukuaye mwanamke kwa haramu amficha watu wasimuone na hajali mahala gani atampatia faragha hata kama kwenye zizi la wanyama katika udhalilifu mkubwa. Hii ndiyo tofauti baina ya halali na haramu, na utiifu na uasi. Ukisema lakini watu wengi hawajali kuyafanya mambo hayo wayafanya nao wacheka bali wajisifu basi nitakujibu kuwa watu hao ni kama wanyama, Allah Subhanahu Wataala ametoa heshima na sharafu katika nyoyo zao kwa hivyo hayachukuliwi mafunzo kutokana na watu kama hawa kwani wao ijapokuwa wengi lakini ni duni.



Ni karama (heshima) aliyowakirimu Allah Subhanahu Wataala Umma wa Mtume Muhammad Salallahu Alayhi Wasalam kwa ulimi wa Mtume wao. Imekuja karama hii katika sunna tatu:- Kauli, Vitendo na akiwaona watu wanaonyoa au kupunguza basi huwakataza. Na ameishi Mtume Salallahu Alayhi Wasalam mpaka kufa kwake bila ya kuzigusa (kukata au kunyoa) ndevu zake na Masahaba wakafanya hivyo hivyo wakafatiwa na Matabiina na waliokuja baada yao katika watu wema bali hata waovu (zamani ilikuwa aibu kubwa kwa mwanamme kunyoa bali hata kukata ndevu).

Kukata ndevu, wacha mbali kuzinyowa, ni haramu kwa mtu mwema na aibu kwa mtu muovu mpaka ukatuingilia na kutupiga vita ukoloni na ukapandikiza ndani yetu mbegu za udhalilifu na kutokuwa na sharafu aina mbali mbali. Na wakati wanapoondoka hao wakoloni waacha nyuma yao utekaji wa kifikira yaani zinakuwa fikira za watu wa hiyo nchi zimeathirika na hao wakoloni na hufata mambo yao mabaya. Inakutosha udanganyifu mkubwa waliouleta wa kumpa mwanamke wa Kiislamu uhuru wake akabakia huyu maskini (mwanamke) kapotea hajui nini chakufanya yuko baina ya kutaka huo uhuru wanaojidai nao na uhuru wa kweli ulioletwa na sheria ya Kiislamu akawa kama kondoo anapelekwa na mchinjaji wake kwenda kumchinja naye akimbia nyuma yake amfuata au ayaona malisho ataka kuyaendea kwenda kula lakini huko angojewa na mbwa mwitu apate kumla kabakia yuko katikati hajui nini la kufanya.


                       البقرة: ١٥٦

"Hakika sisi ni wa Allah, na kwake Yeye tutarejea (atatupa jaza yake)."


Nimemgombeza mtu mmoja (Mu-Omani) kwa kunyoa ndevu zake akanijibu nimewaona wanavyuoni na wazee wanyoa ndevu zao. Nikamwambia: Kama ingekuwa kila Mwanachuoni na kila mzee astahiki kuigwa basi wa kwanza mwenye haki ya kuigwa angelikuwa Ibliis. Yeye ni mkubwa wa wanavyuoni na mkubwa wa wazee.


Na Allah Subhanahu Wataala ndie Anayeongoza kwenye njia iliyonyooka.



Yamesemwa maneno haya na Samahat Sheikh Ahmed bin Hamad Al-Khaliliy – Mufti Mkuu wa Oman:

Suali :  Baadhi ya Waislamu waasi husema kuwa hakuna katika Uislamu maelezo ya uwazi (katika Qurani na Sunna) ya kuharimisha ulevi na sigara. Nini jawabu la mtu kama huyu. Tafadhali kwa kutufahamisha.


Jawabu:  Ni neno kubwa hilo alilolisema huyu mzushi muongo na umekuwa uzushi mkubwa juu ya Allah Subhanahu Wataala na Mtume wake Salallahu Alayhi Wasalam na Dini yake kwa kuwa kuharimishwa kwa ulevi ni wazi na thabiti kwa Aya za Qurani ambazo hazina shaka ambazo hazitilii shaka isipokuwa wale waliokuwa wameachwa hawapewi msaada wala ushindi (na Allah Subhanahu Wataala na Mtume wake Salallahu Alayhi Wasalam na Waumini) ambao wametiwa upofu na mapendekezo ya nafsi zao, zikiwapeleka kwenye hilaki. Vipi mtu aweza akadai kitu hicho na Allah Subhanahu Wataala amesema katika sura ya Al-Maida:


                                                                           ﭱﭲ           المائدة: ٩٠ - ٩١

"Enyi Mlioamini! Bila shaka ulevi na kamari na kuabudiwa (kuombwa) asiyekuwa Allah na kutazamia kwa mishare ya kupiga ramli (na vinginevyo); (yote haya) ni uchafu (ni) katika kazi za shetani. Basi jiepusheni navyo, ili mpate kufaulu (kutengenekewa). Hakika shetani anataka kukutilieni uadui na bughudha baina yenu kwa ajili ya ulevi na kamari; na anataka kukuzuieni kumkumbuka Allah na (kukuzuieni) kusali. Basi je! Mtaacha mambo hayo?."


Basi kuharimishwa kwa ulevi katika Aya mbili hizi (zilizotajwa juu) kuko wazi kabisa katika pande kumi:-


Wa kwanza:  Umewekwa ulevi pamoja na kamari, nayo ni kula mali ya mwingine bila ya haki.


Wa Pili:  Umewekwa ulevi pamoja na kuabudiwa asiyekuwa Allah na kutazamia kwa mishare ya kupiga ramli, na yote hayo ni katika njia za ushirikina na amali za washirikina.


Wa tatu:  Kuhukumu kuwa huo (ulevi) ni uchafu na uchafu hauwi halali.


Wa nne:  Kubainisha kuwa huo (ulevi) ni katika vitendo vya shetani, na vitendo vyake si miongoni ya vilivyokuwa halali katu.


Wa tano: Kuamrishwa kuacha kuunywa, na amri (ya Allah) ni wajibu kuitekeleza ikiwa hakuna kilichokuja kuivunja hiyo amri.


Wa sita:  Uokovu umeambatanishwa na kuacha ulevi.


Wa saba:  Hakika ni katika sababu za uadui na uchukivu. Na kinachosababisha uadui na kuchukiana baina watu basi ni haramu.

Wa nane: Imebainishwa kuwa (ulevi) unazuia kumtaja Allah na kinachozuia kumtaja Allah basi ni haramu.


Wa tisa:  Imebainishwa kuwa (ulevi) unazuia kusali ambayo ndiyo kichwa cha ibada zote na mkusanyiko wa kumkumbuka (Allah) na ndio inayojenga uongofu katika kheri.


Wa kumi:  Kusisitiza wajibu wa kuuacha (ulevi) na kukoma kuunywa kwa maneno makali sana nayo ni maneno yake Allah Subhanahu Wataala:


       المائدة: ٩١

 “Basi jee! Mtaacha mambo hayo.”


Basi laiti nijue kitu gani kimebakia (baada ya dalili zote hizo juu) kwa huyu anaedai kuwa hakuna dalili katika Uislamu ya kuharimishwa ulevi. Na katika hadithi sahihi kuna dalili zinazoshikamana kuonesha uharimisho wa ulevi.


Katika hizo kauli yake Salallahu Alayhi Wasalam:

كل مسكر خمر وكل خمر حرام ) )

‘Kila kinacholewesha ni ulevi, na kila ulevi ni haramu’


Na kauli yake Mtume Salallahu Alayhi Wasalam:

ما أسكر كثيره فقليله حرام ))

‘Kinacholewesha wingi wake basi uchache wake ni haramu’


Na kauli yake Salallahu Alayhi Wasalam:

 ( حرام قليله ما أسكر كثيره )

'Ni haramu uchache wake kinacholewesha wingi wake’


Na kauli yake Salallahu Alayhi Wasalam:

ما أسكر الفرق منه فملء الكف منه حرام )   )

‘Kinacholewesha wingi wa “Al-Faraq” (uzito wa ratili kumi na sita)  basi gao lake (mjazo wa kiganja) ni haramu.'


Na kauli yake Salallahu Alayhi Wasalam:

لعن الله الخمر و شاربها...) )

"Allah Ameilaani pombe na mwenye kuinywa…"

Hadithi hizi zimeenea na zimekubaliwa na Umma kwa hiyo hakuna nafasi ya shaka.


Ama sigara watu hawakuwa wakiitumia wakati ulipoteremshwa Ujumbe wa Uislamu bali imekuja baada yake kwa makarne mingi. Kwa hivyo kukatazwa kwake kunaingia katika misingi ya ujumla iliyowekwa na Uislamu ya halali na haramu, kwani Uislamu unaharamisha moja kwa moja kila kinachodhuru akili, mwili, mali au heshima. Na madhara ya kuvuta sigara yapatikana katika mambo yote hayo yaliyotajwa juu bila ya kuhitaji maelezo zaidi. Kuwa sigara inasababisha maradhi mabaya yanayoua ya kansa (Cancer) peke yake inatosha kuiharamisha. Tunamuomba Allah Subhanahu Wataala atukinge nayo. Amin. Kwani (hiyo sigara) ni mshare uuao na nani ambaye anayeruhusu kuiua nafsi yake licha ya harufu yake kuwa mbaya na Allah Subhanahu Wataala anasema:


             الأعراف: ١٥٧

“Na anawahalalishia vizuri na kuwaharamishia vibaya”.


Kwa hivyo sigara ni haramu iliyo wazi kwa dalili hizo, na anaebisha basi huyo anaipinga akili yake mwenyewe na anakataa uhakika wa mambo. Tunamuomba Allah Subhanahu Wataala atuepushe na hali hiyo na yeye Mola ndiye Mjuzi wa kila kitu.

Na kutimia kwa fatwa hii ndio kumalizika kwa makala hii. Namshukuru Allah Subhanahu Wataala kwa taufiki yake. Na Rehema na Amani ziwe juu ya Mbora wa Mitume - Mohammad na Jamaa zake na Masahaba zake wote. Hakuna uwezo wala nguvu isipokuwa kwa Allah Mtukufu Mkubwa.




[1] Hii ni kwa rai ya baadhi ya maulama; wengine wanasema sala ya sunna kabla ya fardhi ya alasiri haikuthibiti, na hii ndiyo aliyoisahihisha Alimu wa Hadithi Sheikh Said bin Mabrouk Al-Qannubi katika kipindi cha Sual Ahli-'Dhikri cha TV ya Oman, kisha akasema lakini hakuna dalili kuwa inakatazwa kusali nafla kabla ya fardhi ya alasiri kwa anayetaka, kutokana na kauli ya Mtume –rehma za Allah na amani zimshukie- "Baina kila adhana mbili (yaani adhana na iqama) kuna salaa".

No comments:

Post a Comment

Note: only a member of this blog may post a comment.